RAIS wa Tanzania, John Pombe Magufuli, amempigia chapuo Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa wananchi wa Jimbo la Kilosa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilosa … (endelea).
Leo Jumatatu tarehe 29 Juni 2020 wakati akizungumza na wananchi wa wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, Rais Magufuli amesema Profesa Kabudi amezaliwa wilayani humo na kumtaka waziri huyo kujitokeza katika mkutano huo, ili awasalimia ndugu zake.
Hata hivyo, Waziri Kabudi hakuwepo katika mkutano huo.
“Nina ambiwa kuna mtu mmoja amezaliwa hapa hapa, Profesa Kabudi, si ndio,” alisema Rais Magufuli kasha wananchi wakaitikia kwa sauti kubwa ya kushangilia
Alikuwa anazungumzia migogoro iliyokithiri ya ardhi Kilosa akisema, ndiyo wilaya inayoongoza kwa migogoro ya ardhi nchini na akasema kama kungekuwa na mbunge makini angeweza kulifanyia kazi.
“Lakini tatizo lenu ninyi watu wa huku, muwe mnaangalia, munachaguaga kwa jazba, mnachagua watu ambao saa nyingine hawawasaidii,” amesema Rais Magufuli.
Baada ya kauli hiyo, Rais Magufuli aliwauliza wananchi mbunge wa hapo anato chama gani, wakamjibu kwa sauti ‘CCM’ kisha Rais Magufuli akasema, “Kabudi hebu njoo usalimu ndugu zako hapa, Profesa Kabudi yupo hapa, ameenda kwenye kikao? nilitaka aje awasalimu ndugu zake.” Mbunge huyo ni Mbaraka Bawazir.
Baada ya kueleza hayo, Mohamed Said Makala, mwananchi wa Kilosa alinyanyuka na kushika kipaza sauti baada ya kupewa ridhaa na Rais Magufuli.
Makala amemwomba Rais Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), ahakikishe Profesa Kabudi anapitishwa na CCM kugombea jimbo hilo, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.
“Prof. Kabudi ni mzaliwa wa hapa, na amesomea hapa mimi naomba mumpatie kura, naomba baraza lako la NEC (Halmashauri Kuu ya CCM Taifa) umpitishe,” amesema Makala.
Prof. Kabudi ameingia katika Baraza la Mawaziri la Serikali ya Awamu ya Tano, baada ya kuiteuliwa na Rais Magufuli kuwa mbunge.
Awali, aliteuliwa kuwa Waziri wa Katiba na Sheria, kisha baadae kuhamishiwa wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Leave a comment