RAIS wa Tanzania, John Magufuli, amelipongeza Bunge la nchi hiyo, kwa kupitisha azimio itakayozuia mtu au mamlaka kuhamisha Makao Makuu ya nchi yaliyopo Dodoma kwenda eneo jingine. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Rais Magufuli ametoa pongezi hizo leo Alhamisi tarehe 11 Juni 2020 wakati akihutubia katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya lami kwenye mji wa Serikali, ulioko Mtumba jijini Dodoma na Jengo la Mamlaka ya Barabara za Mjini na Mjini (Tarura).
“Bahati nzuri nalipongeza sana Bunge pia limeweka kwa kupitisha sheria kabisa kuwa makao makuu ni Dodoma, kwa hiyo hata nikiondoka kuwa rais atakayekuja hatahamisha makao makuu ya Dodoma. Atakaa hapa hapa kwa hiyo ni amri kwamba Dodoma ndio makao makuu,” amesema Rais Magufuli.
Kiongozi huyo wa Tanzania amesema hatua hiyo ya bunge kupitisha azimio la kutambua Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi, inaenzi mawazo ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, ya kuufanya mkoa huo kuwa kitovu cha taifa hilo.
“Baba wa taifa alitangaza Dodoma kuwa makao makuu tangu mwaka 1973, leo zaidi ya miaka 40 na kitu, lakini nataka kuwathibitishia mawazo ya Baba wa taifa yalikuwa safi sana. Lazima tutekeleze yaliyowazwa na muasisi wa taifa hili Julius Kambarage Nyerere,” amesema Rais Magufuli.
Jumatatu ya tarehe 8 Juni 2020, Bunge lilipitisha azimio la kutaka Serikali kutobadili uamuzi wa Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi ya Tanzania na shughuli zake za kiserikali.
Azimio hilo liliwasilishwa bungeni na Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM).
Tayari, Rais Magufuli, Makamu wake, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, wizara na taasisi mbalimbali zimekwisha kuhamia Dodoma.
Leave a comment