RAIS wa Tanzania, Dk. John Magufuli amesema serikali yake itaendelea kuboresha sekta ya afya ili wananchi wapate huduma bora za afya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Shinyanga … (endelea).
Amesema kauli hiyo leo Alhamisi tarehe 28 Januati 2021, wakati anazindua jengo la wagonjwa wa nje katika Hospitali ya Halmashauri ya Kahama, Shinyanga.
Pia ameahidi kuondoa changamoto katika sekta ya afya ikiwemo kuongeza watumishi wa afya, pamoja na kuboresha mazingira ya utendaji kazi wao ili watoe huduma bora za afya.
“Ninajua bado changamoto zipo lakini nataka kuwahakikishia tutaendelea kutoa huduma nzuri, kuajiri watumishi wa afya ili hii sekta ya afya, iweze kutoa huduma nzuri kwa wananchi.
“Serikali yenu ambayo mmeichagua, tutaendelea kuboresha huduma za afya ili watoto na kina baba waweze kunufaika na matunda ya kweli,” amesema Rais Magufuli.
Akizungumza katika uzinduzi huo amesema, hadi sasa serikali yake imeongeza katika bajeti ya Wizara ya Afya, fedha za kununulia dawa kutoka Sh. 31 Bilioni hadi kufikia Sh. 270 Bilioni.
“Na ndio mana tumeongeza hata bajeti kwa ajili ya dawa kutoka Sh. 31 Bil hadi 270 Bil na ndio maana hata upatikanaji wa dawa tunaanza kuboresha zaidi,” amesema Rais Magufuli.

Amesema, katika kipindi cha miaka mitano ya uongozi wake, serikali imeajiri watumishi wa afya 14,000.
“Nafahamu katika kipindi cha miaka 5 tumetoa ajira kwa watumishi wa afya wapatao 14,000 na mwaka jana mwishoni tumeajiri madaktari 1,000.
“Natumai wizara inayohusika itatoa huduma nzuri ili kusudi na ninyi muendelee kufanya kazi,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment