RAIS mstaafu wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, ameongoza maelfu ya wananchi jijini Dar es Salaam, katika ibada ya swala ya maiti ya mwanasiasa mkongwe nchini, Maalim Seif Sharif Hamad. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Ibada hiyo maalum kwa ajili ya marehemu, ilifanyika Msikiti wa Maamur, uliyopo eneo la Upanga, mkabala na hospitali ya taifa ya Muhimbili.
Wengine waliohudhuria ibada hiyo, ni Kiongozi wa chama cha ACT- Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe.
Ibaada ya swala ya maiti ya Makamu wa Kwanza wa Rais Visiwani, iliyoanza majira ya saa 2:30 asubuhi ya 18 Februari 2021, ilimalizika saa 3 na dakika tano.
Maalim Seif (77), alifariki dunia jana Jumatano, saa 5:26 asubuhi, katika hospitali ya taifa Muhimbili, jijini Dar es Salaam.
Taarifa ya kifo chake, ilitangazwa na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi.
Katika taarifa yake kwa umma, Rais Mwinyi alisema, Maalim Seif alifikishwa katika hospitali ya Muhimbili, tokea 9 Februari mwaka huu.
Rais Mwinyi akatangaza siku saba za maombolezo, ambapo amesema, bendera zote zitapepea nusu mlingoti.
Mazishi ya kiongozi huyo shupavu katika mapambano ya demokrasia nchini na Afrika, yanatarajiwa kufanyika jioni ya leo Jumatano, kijijini kwake, Mtambwe, wilaya ya Wete, mkoa wa Kaskani Pemba.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Serikali ya Zanzibar, baada ya kutoka msikitini, mwili wake uliekelea uwanja wa ndege wa Dar es Salaam, kwa ajili ya kusafirishwa kwenda Unguja.
“Mara baada ya mwili kufika Unguja, utapelekwa viwanja vya Mnazi Mmoja, kwa ajili ya ibada ya swala na salam za rambirambi,” imeeleza taifa hiyo.
Aidha, mwili wa Maalim Seif utapelekwa kwenye viwanja vya Gombani, Pemba, kwa ajili ya swala, inayotarajiwa kuanza saa 7 mchana na badaye utasafirishwa hadi kijijini kwake, Mtambwe, kwa ajili ya mazishi.
Leave a comment