BAADA ya miaka 30 kupita pasina uongozi wa juu wa Zambia kualikwa White House ya Marekani, hatimaye Rais mpya wa Taifa hilo, Hakainde Hichilema ametinga Ikulu hiyo inayoongozwa na Joe Biden. Anaripoti Patricia Kighono, TUDARCo … (endelea).
Ni baada ya kualikwa na Makamu wa Rais wa Marekani, Kamala Harris na kufanya mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kwenye nyanja za afya na utayari wa kukabiliana na majanga.
Hichilema ambaye alikuwa kiongozi wa chama cha upinzani cha United Party For National Development (UPND), aliingia rasmi Ikulu ya Zambia Jumanne ya tarehe 24 Agosti 2021, baada ya kumshinda Edger Lungu.
Lungu aliyekuwa Rais wa Zambia, alishindwa kutetea nafasi hiyo katika uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 12 Agosti 2021 kwa kupata kura milioni 1.8 huku Hichilema akipata kura milioni 2.8.
Rais Hichilema ambaye yupo Marekani kuhudhuria mkutano wa 76 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UN), jana Jumatano tarehe 22 Septemba 2021, alipata fursa ya kualikwa White House ya Marekani, inayoongozwa na Rais Joe Biden.
Katika sehemu ya video iliyowekwa mtandaoni yenye dakika 5:12, Makamu wa Rais wa Marekani, Kamala Harris alisema “nina furaha kubwa kukukaribisha Rais (Hichilema) katika Ikulu ya White House na hii ni mara ya kwanza kumkaribisha Rais wa Zambia White House tangu mwaka 1992, hii ni historia kubwa.”
Aliyepata fursa hiyo ya kufika White House katika kipindi hicho ni Baba wa Taifa wa Zambia, Hayati Keneth Kaunda.
Kamala alimpongeza Hichilema kwa kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Zambia na kumtaka kuhakikisha anasimamia vyema masuala ya utawala bora, haki za binadamu, demokrasia na kufanya mabadiliko makubwa ya kuinua uchumi wa Taifa hilo.
Kamala alitumia nafasi hiyo kumweleza Rais Hichilema kwamba yeye aliwahi kutembelea Zambia akiwa na miaka mitano jambo ambalo liliibua furaha kwa wawili hao wakati wakizungumza kile walichokubaliana.
Kwa upande wake, Rais Hichilema amempongeza kwa kumwalika “nashukuru sana kwa kunialika baada ya kipindi kirefu kupita bila kualikwa. Nashukuru sana.”
Rais Hichilema alisema katika kipindi chake cha uongozi atahakikisha anazingatia utawala wa kisheria, kuimarisha taasisi, demokrasia na kuinua uchumi wa nchi.
“Bila kufanya hivyo kwa kuimalisha demokrasia na uchumi. Hili ndilo limewafanya wananchi wa Zambia wakiwemo vijana kutupa fursa ya kuongoza na sisi tutawatumikia,” alisema Rais Hichilema
Katika kuonesha anabana matumizi, Rais Hichilema alikwenda kuhudhuria mkutano huo nchini Marekani kwa kutumia ndege ya abiria badala ya ndege binafsi ya rais huku akiwa ameambatana na msafara wa watu watatu pekee.
Hichilema alisafiri tarehe 19 Septemba kuelekea jijini New York kushiriki mkutano huo ambapo alitoa nene moja kuu kwa kupanda ndege ya Shirika la Ndege la Qatar akisema mpangilio wa safari yake umelenga kubana matumizi.
“Tunakwenda New York kushiriki Mkutano Mkuu wa UN, tunakwenda kushirikiana na wadau mbalimbali na muhimu kwa faida ya nchi yetu. Tumekwenda ujumbe wa watu wachache ili kazi hii iwe na tija na gharama nafuu zaidi kwa taifa letu,” alisema Rais Hichilema.
Leave a comment