RAIS wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (Fifa), Gianni Infantino, ameipongeza timu ya soka ya Simba ya Dar es Salaam kwa kutwaa ubingwa wa ligi kuu Tanzania Bara 2020/21. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Simba imetwaa ubingwa huo mara ya nne mfululizo na Jumapili hii ya tarehe 18 Julai 2021, itakabidhiwa kombe lake katika mchezo wa mwisho, dhidi ya Namungo FC, Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Taarifa iliyotolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), leo Ijumaa tarehe 16 Julai 2021 na Ofisa Habari na Mawasiliano wake, Cliford Mario Ndimbo, imesema Infantino amemtumia barua Rais wa TFF, Wallence Karia.
Katika barua hiyo, Infantino alisema ubingwa ni matokeo ya juhudi na kutekeleza majukumu kwa kila mmoja ndani ya klabu hiyo.
“Naomba uwakilishe pongezi zangu kwa kila mtu aliyehusika katika mafanikio ya Simba na kuwatia moyo waendelee kufanya kazi kwa moyo wa ushirikiano, ari na ushupavu,” amesema Rais Infantino
Pia, bosi huyo wa Fifa amemshukuru Rais Karia na TFF kwa kuchangia maendeleo na ustawi wa mpira wa miguu katika ukanda huu na dunia kwa ujumla.
Leave a comment