RAIS wa Congo-Brazzaville, Denis Sassou-Nguesso (78), amewekwa karantini baada ya watu kadhaa wa karibu naye kuthibitishwa kuwa wana maambukizi ya virusi vya Corona vinavyosababisha ugonjwa wa Covid-19. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rais Sasouu amelazimika kuahirisha ziara yake huko Pointe-Noire, mji mkuu wa kiuchumi wa Congo-Brazzaville.
Ofisi ya rais imesema kwa mujibu wa itifaki za afya zinazotumika nchini Congo-Brazzaville, rais, akiwa ametangamana na mgonjwa wa Covid-19, anatakiwa kuzingatia muda wa kukaa karantini.
Muda wa kukaa karantini haujaainishwa na baraza la mawaziri, ambalo linasema kwamba watu kadhaa katika msafara wa karibu wa rais wa Jamhuri hiyo hivi karibuni wamepatikana na virusi vya Covid-19.
Taarifa hiyo iliyotolewa na Ikulu ya nchi hiyo leo tarehe 20 Disemba, 2021 ni kwamba baada ya uchunguzi, rais huyo alipimwa lakini hakupatikana na virusi vya Corona.
Tangu Desemba 15 rais hajafanya ziara yoyote na mara ya mwisho Denis Sassou-Nguesso kuonekana hadharani huko Brazzaville ilikuwa Jumatano (Desemba 15) wakati wa uzinduzi wa hospitali kuu katika sehemu ya kaskazini mwa mji wa Brazzaville.
Lakini siku iliyofuata aliwakilishwa na Waziri wake wa Mambo ya Nje, Jean-Claude Gakosso, katika mkutano kati ya Uturuki na Afrika mjini Istanbul.
Pia aliahirisha ziara iliyokuwa imepangwa kufanyika jana na hadi kesho Jumanne huko Pointe-Noire (kusini).
Hivi karibuni Congo-Brazzaville ililegeza masharti kadhaa ya kudhibiti ugonjwa wa Covid-19, hasa kwa kuidhinisha kufanyika sherehe za harusi. Nchi hiyo tayari imerekodi takriban vifo 360 vilivyosababishwa na Covid-19.
Leave a comment