RAIS wa Malawi, Dk. Lazarus Chakwera amewataka viongozi wa Bara la Afrika, kuinga uongozi uliotukuka wa aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati John Pombe Magufuli. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Amesema, misimamo yake katika kuiongoza Tanzania, imeonyesha nchi za Afrika, zinaweza kufikia malengo pasina kufuata matakwa ya taasisi mbalimbali za kifedha, ambazo zimekuwa zikiwaumiza.
Dk. Chakwera, amesema hayo leo Jumatatu, tarehe 22 Machi 2021, katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma wakati wa shughuli ya kuagwa kitaifa kwa mwili wa Dk. Magufuli.
Mwili wa Dk. Magufuli, utazikwa Ijumaa hii ya tarehe 26 Machi 2021, nyumbani kwao, Chato mkoani Geita.
Rais Chakwera amesema, hivi karibuni, Dk. Magufuli alimwandalia chakula Ikulu ya Dar es Salaam na kesho yake, “akanisindikiza uwanja wa ndege, sikujua kama ilikuwa siku ya mwisho kuona naye na alikuwa akiniaga.”
Amesema, enzi za uhai wake, Dk. Magufuli, alikuwa akipambana na uvivu pindi alipouona na palepale bila alichukua uamuzi pasina kusubiri muda upite.
“Waliposema miradi mikubwa ya miundombinu haiwezi kukamilishwa kwa wakati, walimwona Magufuli akifanya. Kila mmoja ameona na hakutaka kufuata maelekezo ya taasisi za kifedha ambazo zimekuwa zikiacha Afrika na madeni makubwa,” amesema Rais Chakwera.
“Maisha yake ya utumishi wa mfano, kwetu sisi tuliokuwa na heshima ya kuishi hapa duniani, Dk. Magufuli aliyoyafanya, itakuwa njia ya kuendesha mataifa yetu na kufikia malengo na utatufanya kuondokana na uzembe.”
“Dk. Magufuli alikuwa shujaa wa Afrika, mwanamageuzi na jina lake sasa lihifadhiwe katika makabati ya Afrika kama alama ya uamuzi sahihi utakaosababisha kuipata Afrika tunayoitaka na maneno yake yatumike maeneo mbalimbali Afrika,” amesema Dk. Chakwera.
Dk. Chakwera, amemhakikishia ushirikiano Rais mpya wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Naye Rais wa Rais wa Zambia, Edgar Lungu amesema “Rais Magufuli, alikuwa rafiki yangu sana sana, ameniuma sana.”
Leave a comment