RAIS wa Nigeria, Muhamadu Buhari ameshinda katika matokeo ya awali ya kinyang’anyiro cha uchaguzi wa urais uliofanyika Jumamosi ya tarehe 23 Februari 2019 nchini humo, kwa kupata kura milioni 15. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Tume Huru ya Kitaifa ya Uchaguzi Nigeria (INEC), Buhari amemzidi kura zaidi ya milioni 4 aliyekuwa mpinzani wake wa karibu, Atiku Aboubakar aliyeambulia kura milioni 11.
Hata hivyo, upinzani nchini Nigeria umeyakataa matokeo hayo. Katika matokeo hayo, chama cha Rais Buhari kimeshinda majimbo 19 kati ya 36 huku chama kikuu cha upinzani nchini humo cha PDP kikishinda majimbo 17.
INEC imeahidi kuyafanyia kazi malalamiko yote ya wapinzani kabla ya kutangaza rasmi matokeo hayo ya uchaguzi.
Asilimia 35 kati ya watu 73 milioni waliojiandikisha kupiga kura walijitokeza kupiga kura katika uchaguzi huo.
Kama INEC haitabadilisha matokeo hayo, Rais Buhari aliyeingia madarakani tangu mwaka 2015 ataongoza tena Nigeria kwa muhula wa miaka minne mfululizo.
Leave a comment