KATIBU Mkuu wa Wizara ya Maji, Profesa Kitila Mkumbo amechukua fomu ya kuomba Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimpitishe kuwania ubunge Ubungo jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
Profesa Mkumbo amekabidhiwa fomu leo Jumatano tarehe 15 Julai 2020 katika ofisi ya wilaya ya Ubungo na Katibu wa CCM Wilaya yhiyo, Sylvester Yared.
Mbunge anayemaliza muda wake wa jimbo hilo ni Saed Kubenea wa Chadema ambaye hakuchukua fomu kuwania ubunge ndani ya chama hicho na haijafahamika kama atagombea kupitia chama kingine katika uchaguzi huo au la.
Mara baada ya kukabidhiwa fomu, Profesa Mkumbo amezungumza na waandishi wa habari akisema ameanza mchakato wa kuwania ubunge kwa kuchukua fomu.
Alipoulizwa kwa nini anautaka ubunge wakati tayari yeye ni katibu mkuu wizara ya maji, Profesa Mkumbo amesema, “ni utumishi kwa umma, utumishi kwa wananchi, kwa hiyo ni nafasi nzuri ya kuwatumikia wananchi katika nafasi nyingine. Katibu mkuu ni ajira lakini suala la ubunge ni suala la uongozi ndiyo maana natafuta nafasi hii.”
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari mbalimbali
Leave a comment