PROFESA Kitila Mkumbo, mgombea ubunge wa Ubungo, Dar es Salaam kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amebainisha vipaumbele kumi atakavyokwenda kuvifanyia kazi endapo atachaguliwa katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Hamisi Mguta, Ubungo … (endelea)
Ameweka wazi vipaumbele hivyo leo Ijumaa tarehe 4 Septemba 2020 wakati akizindua kampeni zake za ubunge katika uwanja wa EPZA Ubungo External.
Profesa Mkumbo amesema, baada ya kukabidhiwa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/25 ameichambua kwa ngazi ya jimbo na kuandaa vipaumbele kumi atakavyohakikisha anavifanyia kazi.
“Tutakuwa na vipaumbele zaidi ya 10. Lakini kipaumbele cha kwanza ni barabara zinazokwenda mitaani katika makazi ya watu.”
“Kipaumbele changu cha tatu ni barabara za mitaani, kipaumbele changu cha tatu ni barabara za makazi ya watu. Hii ni changamoto kubwa kuliko zote Ubungo na ndiyo maana nimeiweka namba moja hadi tatu,” amesema Profesa Mkumbo
Amesema, Ubungo ina zaidi ya barabaraza za mitaani kilomita 100 “na kilomita 33 ndizo zenye lami na asilimia 60 za barabara hazipitiki kabisa. Kuna kina mama wameshindwa kuwahi hospitali kutokana na ubovu wa barabara. Nitakwenda kushughulikia.”
Pia, Profesa Mkumbo amesema, kipaumbele kingine ni mikopo kwa kina mama, vijana na wenye ulemavu.
“Mikopo ina changamoto mbili. Tuna tatizo la utoaji kwa ubaguzi na CCM inapinga ubaguzi na sisi tutatoa kwa wote bila ubaguzi.”
“Pia, kuna suala la elimu ya ujasiliamali inakwama kutokana na kukwama kuirejesha na dawa ya mikopo ni kuirejesha. Hili dawa yake ninayo mkinichagua nitahakikisha inapata ufumbuzi,” amesema
Kipaumbele kingine ni “Changamoto kubwa ni suala la usafi wa masoko. Hakuna vyoo au mtandao wa kuondoa maji taka. Tunahitaji kuboresha ili yawe mazuri na tutasimamia ili kujenga masoko mapya naya kisasa.”
Profesa Mkumbo amesema, kuna changamoto ya shule nyingi zimekubwa na uhaba wa madawati na majengo ambayo atahakikisha anayamaliza akichaguliwa kwa kushirikiana na wananchi na wadau wa maendeleo.
“Lazima tuwe na shule ya sekondari ya kidato cha sita. Haiwezekani Ubungo tukakosa shule ya kidato cha sita. Hili nalo nitakwenda kulifanyia kazi kama mtanichagua,” amesema Profesa Mkumbo aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji
Kuhusu maji amesema, kwa sasa jimbo hilo linapata maji asilimia 90 na hizo asilimia 10 zilizobaki ni miongoni mwa vipaumbele vyake atakavyokwenda kuvifanyia kazi ili jimbo lote liweze kupata huduma hiyo.
Pia, amewaahidi kupigania zabuni ambazo zitakuwa zikipatikana ndani ya jimbo hilo kipaumbele ziwe kwa wananchi wa Ubungo hususan wanawake.
Leave a comment