MSOMI wa masuala ya sheria na utawala nchini Profesa Issa Shivji, ameeleza kukerwa na mwelekeo wa utungaji sheria mbovu kwa maslahi ya wachache. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Miongoni mwa mifano ya sheria mbovu alizotaja ni pamoja na Sheria ya Takwimu ya mwaka 2018, inayomtaka mtu yoyote kutochapisha au kusambaza taarifa au chochote kuhusu takwimu mpaka apate kibali kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
Akizungumza katika kumbukizi ya miaka 16 ya kifo cha Jaji Francis Nyalali ilioandaliwa na taasisi ya Center for Strategic Litigation jijini Dar es Salaam leo tarehe 3 Aprili 2019 amesema, baadhi ya sheria zinatungwa kulenga watu ama kundi fulani.
“Hivi karibuni tumepitisha sheria nyingi mbovu, mfano hii Sheria ya Takwimu ambapo huwezi kufanya uchambuzi wowote wa kitakwimu na kuutoa mpaka upate kibali,” amesema.
Akimzungumzia Jaji Nyalali, Prof. Shivji amesema maisha yake yaenziwe kwa kuheshimu utawala wa sheria na kwamba, mchango wake (Jaji Nyalali) ulikuwa kwenye utawala wa sheria hivyo amelitaka taifa kusimama na urithi huo.
Jaji John Mroso amemuelezea Jaji Nyalali kwamba alikuwa anaumizwa anaposikia mahakama ikikosolewa, hasa kwenye eneo la ucheleweshaji wa kesi.
“Wanasiasa walikuwa wakikosoa suala hilo ambapo ilimuumiza ikapelekea kusafiri kwenda nchini Marekani kwa ajili ya kupata uzoefu wa namna wanaendeshaje kesi,” amesema Jaji Mroso.
Jaji Mroso amesema, Jaji Nyalali ndiye aliyeanzisha mfumo wa kusimamia kesi za masikini bure. “Hakupendezwa na mtu yoyote aliyetaka kuingilia uhuru wa mahakama.”
Jaji Nyalali alihuduma kama Jaji Mkuu wa Tanzania kuanzia Mwaka 1977 hadi 2000 na kufariki terehe 2 Aprili 2003.
Leave a comment