PROFESA Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), amemshauri Rais Samia Suluhu Hassan, katika utawala wake kulenga Tuzo ya Mo Ibrahim. Anaripoi Hamis Mguta, Arusha … (endelea).
“CUF kinapenda kumuomba rais ajiwekee lengo la kupata tuzo ya Mo Ibrahim kwa kujenga demokrasia, utawala bora na keshimu haki za binadamu pamoja na kukuza uchimi shirikishi utakaoweza kuondoa umasikini,” amesema Prof. Lipumba.
Prof. Lipumba ametoa ushauri huo leo Jumatano tarehe 14 Aprili 2021, wakati akitoa maazimio ya Baraza Kuu la Uongozi la chama hicho.
Tuzo ya Ibrahim inalenga kutofautisha viongozi ambao, wakati wa utawala wao ofisini, waliweza kuziendeleza nchi zao, kuimarisha demokrasia na kuheshimu haki za binadamu kwa manufaa ya pamoja ya watu wao, na maendeleo endelevu.
Wagombea wa tuzo hiyo huwa ni wakuu wa zamani wa Serikali wa Afrika, ambao wameondoka madarakani miaka mitatu iliyopita, wakiwa wamechaguliwa kidemokrasia na kutumikia muda wao uliowekwa kikatiba.
Washindi wa awali wa tuzo hiyo ni pamoja na Joaquim Chissano wa Msumbiji (2007), Festus Mogae wa Botswana (2008), Pedro Pires wa Cape Verde (2011), Hifikepunye Pohamba wa Namibia (2014), Ellen Johnson Sirleaf wa Liberia (2017) na Rais wa Niger, Mahamadou Issoufou (2020). Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela alifanywa mshindi wa heshima wa tuzo hiyo mwaka 2007.
Akizungumzia maamuzi ya baraza hilo, Prof. Lipumba amesema “Baraza Kuu CUF linamtakia utendaji uliotukuka Ras Samia Suluhu Hassan na serikali yake.
“Waiongoze nchi kwa kzuingatia Katiba na sheria za nchi, ikiwa pamoja na kuheshimu sheria zinazoruhusu kufanyika mikutano ya hadhara, maandamano halali na kutoa usawa kwa vyama vyote bila upendeleo wala uonevu katika uwanja wa siasa,” amesema Prof. Lipumba.
Kiongozi huyo wa CUF, amemshauri Rais Samia kubadilisha Sheria za Uchaguzi ili Tume Huru ya Uchaguzi ipatikane mapema kwa ajili ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu 2025.
“Mkakati wa Tume Huru ya Uchaguzi uanze mapema kwa kuuzingatia mapendekezo yaliyomo katika Rasimu ya Jaji Warioba.
“Ni vyema sheria ya uchaguzi ikabadilishwa mapema, ili pawe na muda wa kutosha kuandaa chaguzi zitakazokuwa huru na haki katika miaka ijayo,” amesema Prof. Lipumba.
Chama hicho kimemshauri Rais Samia kuongoza nchi kwa kuzingatia misingi ya Katiba na Sheria.
Leave a comment