MWENYEKITI wa Chama Cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba amemtaka Rais Samia Suluhu Hassan, kuwa jasiri akidai kwamba kuna baadhi ya watu hawapendi jitihada zake za kuimarisha demokrasia. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Prof. Lipumba ametoa wito huo leo Jumamosi, akifungua mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja vya Bakhresa jijini Dar es Salaam.
Aidha, Prof. Lipumba amewataka Watanzania kumpa moyo Rais Samia Ili atekeleze majukumu yake vyema
“Inabidi Rais awe jasiri, kuna watu ambao wamezoea vya kunyongwa, vya kuchinja hawaviwezi. Kwa hiyo tusione hivi tukadhani mambo madogo, kuna watu ambao hawataki kuwa na demokrasia katika nchi yetu. Kwa hiyo sisi tunaohitaji demokrasia tuna wajibu wa kumpa moyo aweze kutembea kwenye dhamira yake,” amesema Prof. Lipumba.
Prof. Lipumba amesema Rais Samia anafuata katiba na kuonesha utashi wa kisiasa kwa kufanyia kazi masuala mbalimbali ambayo amekuwa anashauriwa na vyama vya siasa vya upinzani.
Amesema Rais Samia amekuwa msikivu kwa kuondoa zuio la mikutano ya hadhara, lililowekwa na mtangulizi wake Hayati John Magufuli, kuonesha nia ya kufufua mchakato wa katiba.
Aidha, Prof. Lipumba amemuomba Rais Samia ahakikishe tume huru ya uchaguzi inafufuliwa kabla ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024 na Uchaguzi Mkuu wa 2025.
Amemuomba Rais Samia aendeshe nchi kwa misingi ya demolrasia na utawala bora, pamoja na kupambana kwa dhati dhidi ya rushwa, kulinda haki za binadamu ili akimaliza muda wake apate tuzo inayotolewa na Mo Ibrahim kwa Rais anayefanya vizuri akiwa madarakani.
Katika hatua nyingine, Prof. Lipumba amemuomba Rais Samia azidi kuboresha shughuli za biashara na uwekezaji hususan za wazawa.
Leave a comment