WANAWAKE wa Chama Cha Wananchi (CUF), wamemkabidhi Prof. Ibrahim Lipumba, Mgombea wa chama hicho wa Urais wa Tanzania kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28 2020 kiasi cha Sh. 1 milioni kwa ajili ya kuchukua fomu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Prof. Lipumba amekabidhiwa fedha hizo leo Jumamosi tarehe 8 Agosti 2020 Makao Makuu ya CUF Buguruni jijini Dar es Salaam.
Akizungumza baada ya kukabidhi fedha hizo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake CUF-(JUKE), Kiza Mayeye, amesema, wamechukua hatua hiyo wakiamini Prof. Lipumba ndio mgombea pekee atakayeweza kutatua changamoto za kina mama.
“Tumekusanyika sababu wanawake wa CUF tumeguswa na kufurahishwa na Prof. Lipumba kugombea urais Oktoba. Sisi kama wanawake tukasema hapana tumefurahishwa na hili na tunaamini ni mkombozi wa wanawake tumefanya hivyo sababu tuna imani na wewe,” amesema Mayeye.
Magdalena Sakaya, Naibu Katibu Mkuu CUF- Bara amesema Jumatatu tarehe 10 Agosti 2020, chama hicho kitazindua rasmi mpango wa kuchangisha fedha za Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
“Tarehe 10 chama Taifa tunazindua mpango kabambe kuchangia uchaguzi ulioko mbele yetu, tunaomba kina baba kuhakikisha chama hiki cha makabwela chenye sera ya haki sawa kwa wote kuhakikisha tunapata fedha ya kutosha tuingie kwenye uchaguzi tuwe na fedha za kutosha,” amesema Magdalena Sakaya, Naibu Katibu Mkuu CUF- Bara
Prof. Lipumba amewashukuru wanawake hao kwa mchango wao na kuwaahidi kwamba atafanya kampeni za hoja ili washinde uchaguzi huo.
“Nashukuru kwa mchango wenu na nitahakikisha CUF hatuendi kushiriki tu bali tunakwenda kushinda. Hivyo chama chetu kina sera za kuwatajirisha wanawake na walemavu,” amesema Prof. Lipumba.
Prof. Lipumba amepitishwa na Mkutano Mkuu wa CUF kugombea uchaguzi huo huku mgombea wake mwenza akiwa ni Hamida Uwesu.
Leave a comment