KATIKA kuwajengea uwezo wanasiasa wanawake kuhusu matumizi sahihi ya majukwaa ya mitandaoni, Shirika la Pollicy limezindua mtaala unaofahamika kwa jina la ‘Vote Women’ utakaotumika kuwapatia mafunzo madiwani 20 wa Tanzania kwa muda wa miezi mitatu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mtaala huo pia utawawezesha wanawake wa kada mbalimbali kujifunza namna ya kukabiliana na ukatili wanaotendewa mitandaoni pamoja na aina ya maudhui wanayopaswa kuyaweka kwenye akaunti zao ili kukua kisiasa na kupata fursa mbalimbali.
Akifafanua kwa kina kuhusu mtaalam huo kwa madiwani na wadau kutoka taasisi mbalimbali waliohudhuria uzinduzi huo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, Ofisa Miradi Mwandamizi wa Shirika hilo, Irene Mwenda amesema mtaala huo wa ‘Vote Women’ umetokana na utafiti uliofanywa na shirika hilo nchini Uganda mwaka jana baada ya uchaguzi Mkuu wa nchi hiyo kumalizika.
Amesema katika utafiti huo walibaini asilimia 18 ya wanawake walioshiriki uchaguzi huo walitendewa ukatili wa kijinsia mitandaoni.
Amesema ukatili huo ni pamoja na kutukanwa miili yao, kuambiwa maneno ya kashfa, au skendo za kuvujishwa kwa picha zao pamoja na mambo mengine.
“Wanawake wanasiasa walituambia kuwa pamoja na changamoto zote bado kwao wanaona kuna umuhimu wa kuwa na ujuzi wa kuwa salama mitandaoni.
“Pia walisema mitandao haikutengenezwa kuwa rafiki kwa matumizi yao, kwani kuna changamoto za kilugha kwamba hakuna lugha rahisi za Kiswahili au kikabila.
“Vilevile hakuna usalama, kwa sababu kama ungekuwepo vitendo vya kikatili vingechukuliwa hatua,” amesema.
Amesema pia kuna changamoto za kimfumo ambazo zinahitaji mabadiliko ya kisera na kisheria ambayo yanaanza na wanawake.
“Ndio maana tukaamua kuanza na madiwani ambao wapo ngazi za chini kufanya maamuzi,” amesema.
Akifafanua zaidi, Mratibu wa Mradi wa Program ya kifeminia pamoja na uchechemuzi kutoka Shirika la Pollicy, Navina Mutabazi amesema wamezindua ramsu mtaala huo wa ‘Vote Women’ ili kuwajengea uwezo wa kidijitali wanawake wanasiasa ili waweze kutumia mitandao ya kijamii vizuri na kwa usalama zaidi.
Pia waitumie mitandao hiyo kuonesha kazi zao na shughuli zao za kiuongozi.
“Wanawake watakaoshiriki katika mradi huu ni madiwani 20 ambao watakwenda kupatiwa uwezo katika nyanja hiyo ya kidijitali, watapatiwa mafunzo haya kwa njia ya mtandao.
“Mtaala huu utakuwepo mtandaoni, watausoma kwa kipindi cha miezi mitatu na baada ya hapo tutaendelea kuwashirikisha katika shughuli mbalimbali za kidijitali.
“Tunaamini kuwa changamoto wanazopitia zitafutika na kuongeza mwamko wao katika siasa kutokana mtaala huu,” amesema.
Aidha, Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT), Dk. Victori Lihiru anasema mitandao ya kijamii inaweza kutumika kuongeza chachu ya wanawake kuingia katika nafasi za uongozi.
Amesema jitihada bado zinahitaji kwa sababu licha ya Tanzania kuonekana kinara kwa kutoa nafasi kwa wanawake, katika nafasi za chini wanawake hawaonekana.
Mathalani wanawake ambao ni wabunge sasa ni asilimia 36.8 lakini kati yao wanawake ambao ni wabunge wabunge wa kuchaguliwa ni asilimia 9.8 pekee.
“Madiwani ni asilimia 29 lakini ambao ni wa kuchaguliwa kwenye kata ni asilimia 16.5, Serikali za mitaa wale wenyeviti wa vijiji ni asilimia 2.1, kwenye mitaa ni asilimia 12 na vitongoji ni asilimia sita pekee,” amesema.
Amesema hali hiyo inasababishwa na dhana iliyokuwa imejengeka ndani ya jamii kwa mwanamke hajazaliwa kuwa kiongozi bali ni mwanaume pekee ndio maana karibu asilimia 95 ya viongozi nchini ni wanaume.
“Wanawake waliopo kwenye nafasi mbalimbali za kisiasa na kiungozi sasa wamekuzwa kwenye dhana hiyo, hivyo wao wana wajibu wa kukuza kizazi kipya ambacho hakipo katika dhana ya aina hii.
“Mawaziri na wabunge hawa wanatakiwa kuwaonesha mabinti zetu na watoto wa kike kupitia mitandao yao ya kijamii namna wanavyowajibika kwa jamii kupitia maudhui wanayoyaweka mitandaoni. Tunaomba wawe active katika matumizi ya majukwaa haya ya mitandaoni,” amesema.
Hoja hiyo inaungwa mkono na Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya Tangible Tanzania, Geline Fuko ambaye anasema Barani Afrika ni asilimia 24 tu ya wanawake wapo kwenye nafasi mbalimbali uongozi bungeni.
“Hii inatupa picha kwamba wanawake hatuna mwamko wa kuwania nafasi mbalimbali hivyo kampeni imejikita katika kusaidia wanawake kutumia mitandao ya kidijitali katika kufanikisha shughuli zao za kisiasa.
“Lengo ni kuongeza idadi ya wanawake katika siasa pia kuwa na mazingira yatakayowaongezea fursa mbalimbali.
Amesema mtaala huo utawasaidia wanawake kujifunza na kujiandaa katika medani ya siasa.
Pia wanawake watapata fursa ya kujifunza namna ya kufanya kampeni kwenye mitandao, kutengeneza ‘network’ kwenye mtandao, kukusanya fedha kwa ajili ya masuala ya uchaguzi pia watajifunza namna ya kutengeneza maudhui ya mtandao.
“Wanawake waliopo kwenye nafasi mbalimbali watumie mitandao kuonesha ule uwezo wa mwanamke katika utendaji kazi…ninaamini mambo ambayo viongozi wanawake wamekuwa wakiyafanya ni makubwa sana, ukimuangalia Rais Samia Suluhu ameupiga mwingi, hivi majuzi ametunukiwa tuzo kubwa kule Ghana, ametambalika, tutumie kuonesha kazi zetu pia kupata fursa mbalimbali,” amesema.
Aidha, aliyekuwa mgombea udiwani kata ya Nzuguni Dodoma Mjini, Aziza Said (Chadema) amesema mafunzo hayo yaliyopo katika mtaala huo wa Vote Women yatazidi kumjenga na kumsaidia kwenye safari yake ya kisiasa na kiungozi kwa ujumla.
Naye Beatrice Edward ambaye ni Diwani wa Kata ya Upanga (CCM) amesema mtaala huo utamjenga kuendelea kushiriki na kugombea nafasi mbalimbali za kiserikali.
“Utanisaidia kufikia ndoto zangu hii ikiwa nni pamoja na kufanya kampeni za mitandaoni na kunipunguza gharama kipindi cha uchaguzi,” amesema.
Amesema mojawapo ya changamoto mojawapo ambayo amekumbana nayo mitandao kipindi cha uchaguzi ni unyanyasaji wa kijinsia.
“Kwa sababu huwa tunachukuliwa kuwa wanawake hatuna uwezo wa kuwa kiongozi jambo ambalo nalipinga kwa sababu sisi tuna uwezo kama walivyo wanaume… ndio maana hata sasa nchi hii inaongozwa na mwanamke,” amesema.
Wakati Husna Sungura ambaye ni Mwenezi Ngome ya Taifa na Mwenyekiti wa wanawake Ngome ya Pwani kutoka ACT Wazalendo amesema anaishauri serikali kutilia mkazo kwenye sheria ambazo hazimkandamizi mwanamke.
“Pia iendelee kukemea na kutoa elimu ili watu waelewe kwamba mwanamke ana nafasi gani katika jamii na anaweza kugombea nafasi yoyote ili kuondoa haya manyanyaso tunayokutana nayo katika harakati zetu za kisiasa,” amesema.
Leave a comment