MAGARI ya doria yenye askari wa jeshi la polisi, yamewatisha vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kushindwa kuandamana kama walivyokuwa wametangaza, anaandika Hamisi Mguta.
Doria hiyo ilianza jana asubuhi ambapo magari hayo yalionekana yakiwa yanazunguka ofisi za Baraza la Vijana Chadema (BAVICHA) na makao makuu ya chama hicho yaliyopo Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Maandamano hayo yalipangwa kufanyika leo yakipewa jina la ‘Black Thursday’ ikimaanisha kuwa Alhamis nyeusi ambayo yalitangazwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Patrobas Katambi wiki iliyopita.
Julius Mwita, Katibu Mkuu wa Baraza la Vijana Chadema ameiambia MwanaHALISI Online kuwa maandamano hayo yatafanyika kama ilivyopangwa.
“Kwa bahati mbaya Polisi wameshindwa kutujibu kwa barua na leo asubuhi zaidi ya magari 10 yenye polisi wwenye bunduki yamezunguka yanafanya patrol, lakini gharama ya kumtuma mtu kuja kuleta majibu ni ndogo sana kuliko kuzunguka hapa ambayo ni gharama kubwa,” amesema.
Aidha, ameiambia MwanaHALISI Online kuwa “Polisi wanahela nyingi za kuchezea kiasi cha kushindwa kutuma mtu kutuletea majibu, wanaagiza polisi”.
Mwita amesema magari hayo yalikaa takribani dakika 45 huku wengine wakiwa katika ofisi za Bavicha na wengine wakiwa katika ofisi za makao makuu ya chama.
Amesema baada ya kuona hali hiyo wakawasiliana na Kamanda wa Polisi Kanda maalum ya Dar es Salaam, ……Mambosasa kuuliza ni kwanini wametuma askari badala ya kujibiwa kwa barua, kamishna alisema kuwa yupo kikaoni hawezi kuzungumza. Muda mfupi baadaye magari yale yaliondoka eneo hilo.
“Kitendo hiko kinaashiria mambo makubwa mawili, kwanza ni uoga wa polisi kwa sababu barua imebeba vitu vya kweli na wanajua wameshindwa kuyatekeleza ndiyo maana, hawawezi kujibu kwa sababu wanajua wanakiuka sheria na pili ni ubabe kwa sababu wamediriki kutumia gharama kubwa kuagiza watu,” amesema.
Leave a comment