NDUGU wa marehemu Andrew Kiwia, aliyekuwa dereva wa Hiace wamesusa kuchukua mwili wa ndugu yao. Anaandika Mwandishi Maalum … (endelea).
Ndugu hao wameeleza kuwa, sababu za kutotaka kuchukua mwili wa Andrew ni kutaka uchunguzi zaidi baada ya kufa akiwa mikononi mwa Jeshi la Polisi Moshi, Kilimanjaro.
Matukio ya raia kufia mikononi mwa vikosi vya ulinzi yameendelea kutikisa taifa ambapo sasa polisi mkoani Kilimanjaro wanadaiwa kuhusika na kifo cha Andrew.
Ndugu hao wanahitaji kuonana na Kangi Lugola, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kuelezea mazingira ya kifo cha ndugu yao na vijana wake (polisi) wanavyohusika.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa. Andrew akiwa na mwenzake Obasanjo Kitwi walikamatwa Ijumaa saa 5 asubuhi kwa madai ya kukutwa na gongo.
Watu hao walikamatwa wakiwa karibu na stendi ya Kiborlon na kisha kupelekwa katika Kituo Kikuu cha Polisi.
Hata hivyo, taarifa za kifo cha Andrew zilitolewa asubuhi ya Jumatatu wiki hii.
Polisi walidai kuwa, Andrew alipokuwa mahabusu alijinyonga kwa kutumia suruali yake ya jinsi.
Kauli hiyo imepingwa na ndugu wa marehemu wakihoji, iweje ajinyonge kwa suruali yake huku wenzake wamwache na asitoe taarifa.
Pia maiti hiyo imekutwa na jeraha kichwani Jambo ambalo limezidisha utata wakiamini Andrew amekufa kwa kipigo.
Taarifa ya mazingira ya kukamatwa kwake zimeelezwa na polisi kwamba, Andrew alikutwa na chupa ya gongo, hata hivyo ndugu wa marehemu wameeleza kuwa kijana wao alikuwa akinyoana nywele na Obasanjo.
Ndugu wa marehemu wanahoji iweje ndugu yao aingie mahabusu akiwa hai na atoke akiwa maiti?
Leave a comment