JESHI la Polisi limemtaka Hashim Rungwe, Mwenyekiti wa Chama cha Umma (CHAUMMA) kuripoti katika Kituo cha Polisi cha Oysterbay leo tarehe 3 Juni 2019. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Rungwe ambaye ni mwenyekiti wa muungano wa vyama vinane vya upinzani, alipokea wito huo jana tarehe 2 Juni 2019.
Ni muda mfupi baada ya Rungwe kuzungumza na wanahabari kuhusu msimamo wa vyama hivyo kutoshiriki uchaguzi mdogo wa madiwani, uliopangwa kufanyika tarehe 15 Juni 2019 katika kata 32.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa, Rungwe anaitwa polisi kutokana na mkutano wake na waandishi alioufanya jana kwenye Makao Makuu ya chama chake Makumbusho, jijini Dar es Salaam.
Kwenye mkutano wake, Rungwe alisema kuwa, vyama hivyo vinane ambavyo ni Chadema, Chauma, NCCR-Mageuzi, UPDP, CCK, DP, ACT-Wazalendo na NLD havitashiriki uchaguzi huo mpaka pale Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), itakapotekeleza hukumu ya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam ya kutoruhusu wakurugenzi kusimamia uchaguzi.
Alisema kuwa, wakurugenzi hao wamekuwa wakiwaandikia barua kuwaeleza utaratibu wa kuchukua fomu na kurejesha, huku wakitia saini kama wasimamizi wakuu kinyume na matakwa ya kisheria kwa mujibu wa hukumu hiyo.
“Askari wa Jeshi la Polisi wakiwa kwenye magari matatu walifika ofisi ya CHAUMMA baada ya Press Conference ya viongozi wakuu wa vyama vinane vya upinzani, walimpa taarifa kwamba anatakiwa kuripoti Kituo cha Polisi Oyesterbay, tarehe 03 Juni 2019.
“Polisi hao wanadai kuwa, Mheshimiwa Rungwe anahitajika na Mkuu wa Polisi Kinondoni (RPC-Kinondoni), kutokana na mkutano wake na wanahabari.
“Viongozi waandamizi wa vyama hivyo, waliweka msimamo wa pamoja wa kutoshiriki kwenye uchaguzi wa marudio kwenye kata 32 unaotarajiwa kufanyika tarehe 15 Juni 2019 kwasababu, unasimamiwa na wakurugenzi kinyume na uamuzi wa Mahakama Kuu,” ilieleza taarifa ya Tumaini Makene, msemaji wa Cahdema.
Rungwe mwenyewe amethibitisha kupokea wito wa polisi na kwamba, ataitikia kama sheria inavyoelekeza.
Leave a comment