KLABU ya Polisi Tanzania, inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara imezindua rasmi jezi zake ambazo watazitumia kwenye msimu huu mpya ulioanza hivi karibuni wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Uzinduzi huo umefanyika hii leo tarehe 12, Novemba 2021, jijini Moshi ambapo ndio makao makuu ya timu hiyo sambamba na kutumia Uwanja wa chuo cha ushirika kama Uwanja wao wa nyumbani kwa michezo ya Ligi Kuu na kombe la Shirikisho la Azam.
Timu hiyo imezindua jezi aina tatu ambazo zimetengenezwa na kampuni ya Vunja Bei, ambaye ni mzabuni wao mpya wakutengeneza vifaa vyao.
Jezi ya kwanza yenye rangi nyeupe na kuchanganyika na rangi ya bluu kwenye mikono, itatumika kwa michezo ya nyumbani, jezi ya blue itatumika kwa michezo ya ugenini huku jezi yenye rangi ya kijani wataitumia kama jezi namba tatu (Third Kit)
Sambamba na uzinduzi wa jezi hiyo, mkurugezni wa kampuni ya vunja Bei Fred Nganjiro alikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi milioni 104, mara baada ya kushinda zabuni kwenye klabu hiyo.
Kwenye hafla hiyo, viongozi wa timu hiyo walijipambanua kuwa malengo ya timu yao kwa msimu huu kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara ni kumaliza kwenye nafasi tatu za juu.
Mpaka sasa mara baada ya michezo mitano kuchezwa kwenye Ligi Kuu toka kuanza kwa msimu mpya, Polisi Tanzania inashika nafasi ya tatu ikiwa na pointi, nyuma ya vigogo wa soka nchini klabu za Simba na Yanga.
Katika michezo mitano waliocheza mpaka sasa, Polisi Tanzania wamefanikiwa kupata ushindi kwenye michezo mitatu, sare mechi moja na kupoteza mchezo mmoja dhidi ya Simba.
Leave a comment