POLISI Mkoa wa Dodoma nchini Tanzania, limetoa onyo kwa mtu au kikundi cha watu, kutumia tukio la kushambuliwa kwa Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Upinzani nchini humo Chadema, kujipatia umaarufu kisiasa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mbowe ameshambuliwa na watu wasiojulikana usiku wa kumakia leo Jumanne tarehe 9 Juni 2020 akiwa katika makazi yake Area D jijini Dodoma na watu wanaodaiwa kuwa watatu ambao wamemvunja mguu wa kulia.
Kwa sasa Kiongozi huyo wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, anapata matibabu katika Hospitali ya DCMCT Ntyuka Dodoma na Chadema wamesema, wanaendelea na utaratibu wa kumhamishia jijini Dar es Salaam kwa matibabu zaidi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto akizungumzia tukio hilo mbele ya waandishi wa habari amesema, limetokea kati ya saa sita na robo usiku na taarifa wamezitapa saa moja asubuhi.
Muroto amesema, taarifa walizopata ni Mbowe alishambuliwa na watu watatu waliokuwa wamevalia majaketi ambapo baada ya dereva wake kumshusha, “wakati anapandiusha ngazi, alikutana na watu watatu wamevaa jaketi na kumshambuliwa kwa kumkanyaga kanyanga na mateke.”
Amesema, baada ya shambulio hilo, Mbowe alipelekwa hospitalini kwa matibabu.
“Polisi tunafanya uchunguzi wa kina bila kuacha chochote. Kupata ukweli wa tukio hili. Hakuna kitu kitakachoachwa,” amesema Muroto.
“Tukio hili ni kama tukio jingine, linachunguzwa na vyombo. Tukio hili lisitumike vibaya au kisiasa au njia yoyote ya kujiongezea umaarufu kwa mtu au kundi,” amesisitiza kamanda huyo.
Muroto amesema, “wakati tukio hili linachunguzwa ni marufuku kuingilia. Eneo lile lina walinzi na majirani. Tutapata ukweli.”
Amesema, tukio lipo na linachunguzwa na hakuna kitu kitakachoachwa, “Onyo ni watu kutumia tukio hili kama mtaji wa kisiasa.”
Muroto ameonya hamasa ambayo imeanza kujitokeza katika mitandao ya kijamii kushawishiana kukutana katika ofisi za Chadema Dodoma ay nchi nzima, “Polisi iko macho na yoyote atakayekusanyiki atashughulikiwa. Tutamshughulikia kweli kweli.”
Leave a comment