JESHI la Polisi mkoani Tabora limesema litafanya doria ya kuwabaini watu wanaotaka kujinyonga, kisha kuwafikisha mahakamani. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Barnabas Mwakalukwa, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani humo, wakati akizungumza na wanahabari, amesema hatua hiyo itasaidia kukomesha matukio ya watu kujinyonga.
“Basi niwaambie mwaka huu tabia hizo zikome, kwa wale wanaotegemea kujinyonga, sisi tutawakamata kabla ya kujinyonga halafu tutawapeleka mahakamani. Tutaanza kufanya doria kuhakikisha kwamba wote wanaotarajia kujinyonga mwaka huu tuwakamate,” amesema Kamanda Mwakalukwa.
Wakati huo huo, Kamanda Mwakalukwa amewaomba viongozi wa dini, kutoa ushauri nasaha kwa waumini wao, hasa wenye matatizo ya kiafya na migogoro mbalimbali, ili kudhibiti matukio ya watu kujinyonga.
“Na pia tuna waomba viongozi wa taasisi za kidini wafanye doria za kiroho, ili waweze kuzima matukio ya namna hiyo kwa kutoa nasaha na elimu. Pia wale wataalamu wa ushauri nasaha waende kwa watu wenye matatizo ya kiafya, kuchanganyikiwa kwa akili, ili wawape faraja,” amesema Kamanda Mwakalukwa na kuongeza;
“Kwamba pamoja na matatizo waliyonayo ya kiafya , kiuchumi , kisiasa, migogoro ya kijamii na ya kifamilia, bado wana kuwa na nafasi nzuri ya kuwa na maisha bora baada ya kupewa ushauri nasaha, mara nyingine tunapoteza watu muhimu katika ujenzi wa nchi yetu.”
Leave a comment