JESHI la Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limeeleza, Mhandisi Leopord Lwajabe, aliyekuwa Mkurugenzi Msaidizi wa Miradi ya Umoja wa Ulaya (EU) katika Wizara ya Fedha alifariki kwa kujinyonga. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa wakati akizungumza na wanahabari leo tarehe 31 Julai 2019.
Kamanda Mambosasa amesema, uchunguzi wa awali uliofanyika katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, umebainisha kwamba chanzo cha kifo cha Lwajabe ni kujinyonga.
“Mwili wa marehemu ulihamishiwa Muhimbili kwa uchunguzi zaidi na ilibainika kifo cha marehemu kilisababishwa na kujinyonga. Chanzo cha kujinyonga kwake bado kinachunguzwa,” amesema Kamanda Mambosasa.
Aidha, Kamanda Mambosasa amesema, marehemu Lwajabe aliacha Notebook ofisini kwake aliyoandika ujumbe wa mgawanyo wa mali zake kwa familia yake.
“Tarehe 29.07.2019 wafanyakazi waligundua kuwa marehemu aliacha Notebook juu ya meza ofisini kwake ambapo ilikuwa na ujumbe wa mgawanyo wa mali zake kwa familia yake na kwamba, kwenye msiba wake ng’ombe wane wachinjwe,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda Mambosasa ameeleza, mfanyakazi mwenzake na Lwajabe aliwaeleza polisi ya kwamba muenendo wa marehemu ulibadilika kwa kupunguza kasi ya utendaji kazi.
“Hata hivyo, taarifa toka kwa mfanyakazi mwenzake alisema, marehemu alikuwa amepunguza kasi katika utendaji jambo ambalo sio kawaida yake na hata kazi zingine za muhimu alikuwa akimpa kaimu wake kuzifanya,” amesema Kamanda Mambosasa.
Akieleze mazingira ya kupatikana kwa mwili wa Lwajabe, Kamanda Mambosasa amesema, Jeshi la Polisi lilifika eneo la tukio baada ya kupewa tarifa za tukio hilo na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgoza, Mohamed Said (68).
Kamanda Mambosasa amesema, baada ya polisi kufanya uchunguzi eneo la tukio, walibaini kwamba eneo hilo halikuwa na viashiria vyovyote vya kujitetea wakati wa tukio, pia mwili haukuwa na jeraha lolote isipokuwa shingoni kulikuwa na kamba ya nailoni aliyotumia kujinyonga.
Amesema, polisi waliufanyia upekuzi mwili wa Mhandisi Lwajabe na kukuta fedha kiasi cha Sh. 90,000 kwenye mfuko wa suriali upande wa kulia na Sh. 98,000 upande wa kushoto, pochi yenye Dola za Marekani 10 katika mfuko wa nyuma, kitambulisho cha mpiga kura na saa ya mkononi.
“Wananchi waliitwa ili kuutambua mwili ambapo hakuna aliyeweza kuutambua. Baada ya hapo mwili ulichukuliwa na kuhifadhiwa Hospitali ya Wilaya ya Mkuranga kwa utambuzi na uchunguzi wa daktari na kufunguliwa jalada kosa la kujinyonga, na upelelezi uliendelea ikiwa ni pamoja na kuwatafuta wanandugu wa marehemu,” amesema Kamanda Mambosasa.
Kamanda Mambosasa amesema, mnamo tarehe 29 Julai 2019 ndugu wa marehemu Lwajabe walikuja kuutambua mwili wake.
Leave a comment