JESHI la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewataka wafanyabiashara kuacha kuuza silaha kama mapanga, majambia, visu, manati na upinde bila utaratibu wa kisheria, anaandika Pendo Omary.
Simon Sirro, Kamishna wa Polisi leo amewaambia waandishi wa habari kuwa biashara hiyo kwa sasa imeshamiri katika barabara ya Nyerere/Tazara kwenye mataa ya kuongoza magari, Chang’ombe na gerezani hali inayohatari usalama wa watu hususan watumiaji wa barabara hizo.
“Baadhi ya wauzaji wa bidhaa hizo, hutumia fursa hiyo kuwatishia watu wakiwa kwenye magari binafsi na yale ya umma na kuwaibia mali mbalimbali kama simu za mkono, saa, mikoba, pochi na kompyuta mpakato,” amesema Sirro.
Sirro amesema silaha hizo zinatakiwa kuuzwa kwenye maduka yenye leseni na kwamba atakayepatikana akifanya biashara hiyo atachukuliwa hatua kali za kisheria.
“Tarehe 12 Januari mwaka huu, kwenye mataa ya Tazara alikamatwa mtuhumiwa Ngoli Salakani (39), akifanya biashara hiyo. Hatua za kisheria zinachukuliwa dhidi yake,” amesema Sirro.
Leave a comment