ASKARI Polisi nchini Kenya, Koplo Caroline Kangogo, aliyekuwa akitafutwa kwa tuhuma za mauaji ya watu wawili, amepatikana akiwa amefariki dunia kwa kujipiga risasi, nyumbani kwa wazazi wake eneo la Rift Valley. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kangogo, anatuhumiwa kuwaua kwa kuwapiga risasi wanaume wawili kwa nyakati tofauti tarehe 5 Julai 2021, John Ogweno, polisi mwenzake na Peter Ndwiga (32), mfanyabiashara wa eneo la Juja katika Mji wa Nairobi.
Askari huyo, anatuhumiwa kuwaua askari mwenzake, Ogweno eneo la Nakuru kwa kumpiga risasi kisha kutimkia eneo la Juja umbali wa takribani kilomita 200 ambako alitekeleza mauaji mengine ya Ndwigwa.
Ndwingwa anadaiwa kuuawa na Kangogo wakiwa chumbani katika moja ya hotel ambapo baada ya kutekeleza mauaji hayo, usiku wa manane aliondoka huku muhudumu wa hoteli hiyo akimweleza anakwenda kununua kitu dukani. Hata hivyo, hakurudi.
Mara baada ya kutekeleza mauaji hayo, askari huyo wa kike, alitoweka huku polisi wakitangaza kumtafuta askari mwenzao na kuwasisitiza wananchi hususan wanaume kuchukua hatua dhidi yake na kutoa taarifa mara wakimwona.
Mwili wa Kangongo ulikutwa bafuni jana Ijumaa asubuhi, tarehe 16 Julai 2021, baada ya kujiua kwa kujipiga na bastola kichwani ambayo aliondoka nayo wakati akitekeleza mauaji ya watu hao wawili.
Kamanda wa Polisi wa Rift Valley, George Natembeya alithibitisha kupatikana kwa mwili wa askri mwenzao na kuupeleka kuufanyika uchunguzi wa awali kisha kuuhifadhi hospitalini.
Leave a comment