WAKILI nchini Tanzania, Peter Mdeleka, amewasilisha ombi la kufungua kesi ya kupinga utaratibu wa kukiri kosa na kulipa fidia ili kuondolewa mashtaka au adhabu (Plea-Bargaining), katika Mahakama Kuu Ya Tanzania, Kanda ya Arusha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Wakili huyo wa wa Mahakama Kuu ya Tanzania, amewasilisha ombi hilo jana Jumanne tarehe 24 Agosti 2021, katika mahakama hiyo.
Akizungumza baada ya kuwasilisha maombi hayo, Wakili Madeleka alisema dhumuni lake ni kuitaka mahakama hiyo itoe tafsiri ya kisheria juu ya utaratibu huo, kama Plea-Bargaining ni sahihi au si sahihi.
Na kama sio sahihi, mahakama hiyo ikomeshe utaratibu huo kwa madai kuwa unakiuka haki ya watu.
“Tunataka mahakama itafisiri sheria sahihi katika maombi niliyoleta, ili tupate msiammo wa kisheria kwamba kilichofanyika ni sawa na kama sio sawa utaratibu ukomeshwe,” alisema Wakili Madeleka
Wakili huyo alidai, utaratibu wa Plea-Bargaining uliokuwa unafanya na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), aliyepita, Biswalo Mganga, ulikiuka sheria, akidai haukumshirikisha msajili wa hazina mwenye mamlaka ya kupokea fedha za Serikali.
“Sheria ya Plea- Bargaining inasema kama ikihitajika Serikali ilipwe fidia, anayepaswa kulipwa ni msajili wa hazina na hakuna pahala popote tangu utaratibu wa umeanza kufanyika, msajili alikuwa involved kwa maana ya kupokea fidia kwa niaba ya Serikali, hilo ni kosa,” alidai Madeleka.
Madeleka alisisitiza “hivyo nimeleta maombi kwa ajili ya kupinga utaratibu huo uliofanywa na DPP aliyepita, utaratuibu ule ulikuwa si sahihi sababu ulikuwa hauzingatii sheria na ukasababisha madhara. Si tu kwangu lakini wengine wengi walioshtakiwa kwa makosa ya uhujumu na yalikwisha kwa njia ya Plea-Bargaining.”
Alisema ameamua kuwasilisha ombi hilo kwa kuwa yeye ni mhanga wa utaratibu huo, ambaye alilazimika kutoa Sh. 2 milioni, kama Plea-Bargaining dhidi ya kesi ya uhujumu uchumi Na. 40/2020 iliyokuwa inamkabili katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha.
“Nimeleta maombi haya mahakamani ili mahakama iweze kuangalia kile nilichokubalina na DPP kwenye kesi ya uhujumu uchumi Na. 40/2020, ilikuwa sawa mbele ya macho ya kisheria na kama sio sawa mahakama itatoa muongozo sahihi wa kufanya,” alisema Madeleka.
Leave a comment