CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kinaendelea kukimbiwa na baadhi ya makada wake muhimu, tena waliokuwa na mamlaka. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Edward Sembeye, aliyekuwa Katibu wa Baraza la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), leo tarehe 26 Februari 2020, ametangaza kujitenga na chama hicho na kwamba anapumzika siasa.
Mbele ya waandishi wa habari, Sembeye amesema moja ya vitu vinavyokiumiza chama hicho, ni chama hicho kwenda ama kuendeshwa kwa mdundo wa Freeman Mbowe, mwenyekiti wa chama hicho na si Katiba ya Chadema.
“Leo mambo ya Chadema yanaamuliwa kwa mujibu wa kauli na amri za Mbowe (Freeman Mbowe), sio Katiba. Mwenyekiti ameamua kugeuzi chama kuwa mali yake binafsi.
“Lakini tukitoka nje tunawaaminisha umma wa Watanzania kwamba chama hiki ni mali ya Watanzania. Kuna mambo mengine kiuongozi, tunapaswa kuwa na akiba ya maneno,” amesema.
Amesema, kutokana na kutokuwa na umoja na msimamo, matokeo yake wamepoteza hata majiji waliyokuwa wakiyaongoza.
“…tumechukua Jiji la Dar es Salaam, tumechukua Jiji la Arusha, leo tumeyapoteza majiji yote na bado tunawaambia Watanzania kuwa bado tupo imara,…” amesema.
Sembeya ameonesha kukerwa na maneno ya kejeli yanayotolewa na viongozi wa Chadema pia wajumbe wa Kamati Kuu, akisema jambo hilo si la kistaarabu.
“Juzi nimeona mjumbe mmoja wa Kamati Kuu akisema yule aliyehama ni panya,…
“Dhumuni la chama chetu ni kutetea haki za binadamu, kumwita mtu panya kwa sababu ameondoka kwenye chama chako! Kuna watu wameitwa wanaume suruali, mtu huyu ni Mjumbe wa Kamati Kuu,” amesema.
Leave a comment