KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji (PIC) imeridhishwa na usimamizi na utekelezaji wa miradi ya Maji ya Kibamba-Kisarawe na Pugu-Gongo la mboto iliyotekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kwa kupitia fedha za ndani. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hayo yamesemwa leo Alhamisi, tarehe 24 Machi 2022 na Mwenyekiti wa PIC, Jerry Silaa alipoingoza kamati yake kutembelea miradi hiyo akiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Cyprian Luhemeja na Mwenyekiti wa Bodi, Jenerali mstaafu Davis Mwamunyange.
Silaa amesema hali ya usambazaji maji katika Jiji la Dar es salaam na mkoa wa Pwani inaridhisha hususani katika maeneo yaliyokuwa sugu na upatikanaji wa maji kama vile Kisarawe na Pugu.
“Mfano mzuri ni hapa tulipo katika jimbo la Ukonga, ambapo kwa takribani miaka 40 hapakuwepo huduma ya majisafi, lakini utekelezaji wa mradi wa Pugu-Gongo la mboto umemaliza changamoto hiyo iliyodumu kwa muda mrefu,” amesema Slaa ambaye pia ni Mbunge wa Ukonga.
Silaa ameongeza kuwa kwa kasi wanayoenda nayo DAWASA kamati inaamini ifikapo 2025 itakuwa imewafikia Wananchi wote katika eneo lake la kihuduma.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu DAWASA, Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika, katika usambazaji wa maji ili kuhakikisha yanawafikia wananchi wote.
“Tulipokea maelezo kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan kuharakisha usambazaji wa maji kwa wananchi katika maeneo ambayo miradi imekamilika. Lakini pia tumepokea maelekezo ya kamati katika kuharakisha usambazaji wa huduma ya maji na tunaenda kutekeleza hilo kwa kasi,” amesema Mhandisi Luhemeja.
Kwa upande wake, Bakari Utingo, mkazi wa Kata ya Majohe ameishukuru DAWASA kwa kufikisha huduma ya maji katika kata zote za Pugu na kwa sasa maji ni Mengi na ya uhakika. “Nakumbuka mara ya mwisho maji kutoka bombani katika kata yetu ya Majihe ni mwaka 1999, tumekuwa tukitumia maji ya visima na kununua kwa watoa huduma binafsi kwa muda mrefu.
“Tunashukuru sasa tumefikishiwa huduma na DAWASAna niwaombe waendelee na kasi ya kuunganisha huduma ya maji kwa wananchi wengi zaidi,” amesema Utingo DAWASA inatekeleza miradi mikubwa na midogo mbalimbali ili kufikia asilimia 95 ya upatikanaji ifikapo 2025.
Leave a comment