RAIS wa heshima wa Klabu ya Simba SC, Mohamed Dewji ‘Mo’ leo taerehe 22 Julai, 2022 amempongeza kiungo mshambuliaji wa timu hiyo kutoka nchini Senegal, Pape Osmane Sakho kwa kuibuka mshindi wa goli bora la Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Pongezi hizo za Mo zimekuja baada ya Sakho kushinda tuzo hiyo usiku wa kuamkia leo katika hafla maalum ya Shirikisho iliyofanyika mjini Rabat nchini Morocco.
Kupitia ukurasa wake wa Twitter, Mo Dewji amempongeza kiungo huyo aliyesajiliwa Simba SC mwanzoni mwa msimu uliopita, huku akimshukuru kwa kuiheshimnisha Msimbazi na nchi ya Tanzania.
“Wanasimba na Watanzania tunajivunia mafanikio yako mchezaji wetu Pape Sakho. Hongera kwa kushinda Tuzo ya Goli Bora la CAF 2022 na asante kwa kuleta heshima ya kipekee kwa Simba na Tanzania. Tuzo hii imezidi kuonyesha namna gani Simba ni timu kubwa na ina wachezaji wenye viwango vikubwa! #nguvumoja,” ameandika Mo Dewji.
Wanasimba na Watanzania tunajivunia mafanikio yako @ousmane10_sakho. Hongera kwa kushinda Tuzo ya Goli Bora la CAF 2022 na asante kwa kuleta heshima ya kipekee kwa Simba na Tanzania. Tuzo hii imezidi kuonyesha namna gani Simba ni timu kubwa na ina wachezaji wenye viwango. pic.twitter.com/nEeid1yP6x
— Mohammed Dewji MO (@moodewji) July 22, 2022
Sakho aliingia kwenye kinyang’anyirio cha kuwania Goli Bora la CAF 2022 kupitia bao alilofunga kwa ufundi wa kipekee mabingwa wa Ivory Coast- ASEC Mimosas katika mchezo wa hatua ya Makundi Kombe la Shirikisho Barani humo msimu wa 2021-22.
Mchezo huo uliopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam, Simba SC ikiibuka na ushindi wa mabao 3-1 huku mabao mengine yakifungwa na Shomari Kapombe na Peter Banda.
Mabao mengine ambayo yaliingia kwenye kinyang’anyiro cha kuwania Goli Bora la CAF 2022 yalifungwa na Gabadinho Mango wa Orlando Pirates ambapo bao lake alilifunga akiwa kwenye majukumu ya timu ya taifa ya Malawi dhidi ya Morocco kwenye Fainali za Mataifa ya Afrika AFCON 2022 zilizopigwa nchini Cameroon mwanzoni mwa mwaka huu 2022.
Zouhair El Mountaraji wa Wydad Athletic Club naye aliingia kwenye kinyang’anyiro hicho kwa bao lake alilofunga kwenye mchezo wa Fainali ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika dhidi ya Al Ahly mwezi Mei.
Leave a comment