KIONGOZI wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis amewateua mapadre, Henry Mchamungu na Stephano Musomba, kuwa Maaskofu wasaidizi Jimbo Kuu la Dar es Salaam, nchini Tanzania. Anaripoti Ibrahim Yamola…(endelea).
Uteuzi huo, umetangazwa leo Jumatano, tarehe 7 Julai 2021 na Askofu Mkuu, Jude Thaddeus Ruwa’ichi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, katika misa takatifu ya upadrisho kwa mapadre 14, iliyofanyika viwanja vya Msimbazi Center.
Mara baada ya kumaliza kuwapa daraja hilo takatifu, Askofu Mkuu Rwa’ichi alisema Baba Mtakatifu, Francis amewateua Mapadre Mchamungu na Musomba kuwa maaskofu wasaidizi.
Kisha Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padre Charles Kitima akatoa taarifa rasmi ya uteuzi huo akisema, Askofu mteule, Mchamungu, alizaliwa tarehe 18 Januari 1965, Legho Kilema, jimbo la Moshi, Kilimanjaro.
Amesema, baada ya masomo yake ya upadre, alipewa daraja takatifu la upadre tarehe 24 Juni 1994 na kuhudumu katika nafasi mbalimbali za utume Jimbo Kuu la Dar es Salaam na TEC.
Hadi anateuliwa kuwa Askofu mteule, Mchamungu alikuwa Mwalimu na mlezi wa seminari ya Segerea, Dar es Salaam.
Padre Kitima amesema, Askofu mteule Musomba, alizaliwa tarehe 25 Septemba 1969, Malonji Jimbo la Mbeya.
Baada ya masomo ya upadre, alipewa daraja takatifu la upadre tarehe 24 Juni 2004 na kuhudumu katika nafasi mbalimbali za uteme shirikani na Jimbo Kuu la Dar es Salaam na Morogoro.
Hadi uteuzi wake, Askofu mteule Musomba alikuwa Paroko wa Parokia ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili- Mavurunza, Dar es salaam na Katibu wa Shirika lake la Waangustiniani Kanda ya Tanzania.
Leave a comment