CARLO Maria Vigano, Mjumbe wa zamani wa Vatican amemtaka Papa Francis, Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani kujiuzulu kufuatia kadhia inayoliandama kanisa hilo ya mapadri wake kutuhumiwa kuwafanyia ukatili wa kingono watoto wadogo. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Wito huo umetolewa na Askofu Mstaafu Vigano ikiwa imepita siku moja tangu Papa Francis kuomba msamaha kwa Mungu kuhusu kadhia hiyo, alipotemebelea nchini Ireland.
Hivi karibuni Ripoti ya Washauri wa Mahakama ya Marekani ilidai kuwa, zaidi ya mapadri 300 waliohusika na unyanyasaji wa kingono waliwaharibu watoto 1,000 katika dayosisi sita za Pennsylvania katika kipindi cha miaka 70.
Katika tamko lake lenye kurasa kumi na moja, Askofu Mstaafu Vigano alikumbushia tukio la Papa Francis la kumuondolea adhabu Mc Carrick, Askofu wa zamani wa Washngton DC aliyopewa na Papa Benedicto wa kumi na sita kutokana na utovu wa nidhamu, licha ya uwepo wa ushahidi unaoonyesha tabia mbaya na utovu wa nidhamu aliyowafanyia baadhi ya waseminari na mapadri.
Vigano alisema mnamo mwaka 2013 alizungumza na Papa Francis binafsi kuhusu adhabu hiyo na jinsi Mc Carrick alivyowapotosha waseminari na mapadri wengi.
“Katika wakati huu mgumu kwa kanisa anapaswa akubali makosa yake na kwa kuzingatia kanuni ya kanisa ya kutovumilia kabisa makosa haya, Papa Francis anapaswa awe wa kwanza kutoa mfano kwa makadinali na maaskofu waliomkingia kifua Mc Carrick kwa kujiuzulu pamoja nao,” amesema.
Hata hivyo, Vatican haikutoa maoni na au kupinga juu ya madai hayo ya Askofu Mstaafu Vigano.
Leave a comment