MAKAMU wa kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othuman Masoud Othuman amekishukuru chama chake cha ACT-Wazalendo kwa kumpendekeza kwenye nafasi hiyo huku akiwaahidi kuwatumikia pasina kuchoka. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Othuman, ametoa shukruni hizo leo Jumamosi, tarehe 19 Juni 2021, katika kikao cha Kamati Kuu ya ACT-Wazalendo, kinachofanyikia Hoteli ya Lamada, Ilala jijini Dar es Salaam.
Amehudhulia kikao hicho kwa mara ya kwanza, tangu alipoapishwa tarehe 2 Machi 2021 na Rais wa Zanzibar, Hussein Ali Mwinyi kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais, kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Hayati Maalim Seif Sharif Hamad.
Maalim Seif, aliyekuwa mwenyekiti wa ACT-Wazalendo alifikwa na mauti saa 5 asubuhi ya tarehe 17 Februari 2021, katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam, alipokuwa akipatiwa matibabu.
Mara baada ya kifo hicho, ACT-Wazalendo ilipendekeza jina la Othuman kwa Rais Mwinyi kujaza nafasi hiyo ambapo kiongozi huyo wa visiwa hivyo, alimteua Othuman kisha kumwapisha.
Leo Jumamosi, katika kikao cha kamati kuu kinachoongozwa na Kaimu Mwenyekiti, Dorothy Semu kabla ya kuanza, walimkaribisha Othuman kuzungumza ikiwemo kuvalishwa taji la kuashirikia kuwa mjumbe wa kikao hicho.
Huku mapofi yakipigwa na wajumbe wa kikao hicho, Othuman amesema “nashukuru sana na hatimaye nimekuwa mjumbe wa kamati kuu.”
“Nakishukuru sana chama changu kwa vile kimenifanya kufika hapa, tumeondokewa na mzee wetu, mimi nilipenda kumwita tajiri yetu, alikuwa kila kitu.”
“Ameondoka pamoja na watu wooote ndani ya chama wanaoweza kushika nafasi hii lakini mkaniona mimi nafaa. Hii ni dalili ya wazi kwamba tumehitimu lile tulilokuwa tunalisema la umoja na mshikamano.”
Othuman aliyewahi kuwa mwanasheria mkuu wa Zanzibar amesema “bila umoja na mshikamano, mwingine anaona ni jambo lahisi tu lakini ulikuwa ni mtihani ambao taasisi, jamii, mataifa yanafeli huu mtihani lakini sisi tuliufaulu na hakuna hata mmoja alidhania na ni dalili ya ukomavu kwa viongozi wa chama chetu bila kuparanganyika na tukabaki pamoja.”
“Jukumu mlilonipa ni kubwa sana, lakini ile imani mliyonipa ni kubwa sana,” amesema
Akihitimisha salamu zake, Othuman amesema “sina kikubwa cha kuwalipa ila imani kwa kukitumia chama chetu na nchi yetu kwa kiwango bora zaidi na pale nitakapoona sitaweza kufikia malengo ndiyo ubinadamu na mnisamehe na mnielekeze.”
Leave a comment