SERIKALI imewaagiza wakuu wa mikoa (RC) na wa wilaya (DC), waandae mikakati ya kudhibiti maambukizi ya wimbi la tatu, la ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (Covid-19). Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Jumamosi, tarehe 10 Julai 2021 na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Dorothy Gwajima, alipofanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
Waziri huyo wa afya, amewataka wakuu wa mikoa na wilaya, kuzingatia miongozo ya kujikinga na kupambana na Covid-19, iliyowekwa na Serikali, kwa ajili ya kudhibiti mlipuko wa wimbi hilo la tatu.
Dk. Gwajima ametoa agizo hilo, baada ya kubaini ongezeko la idadi ya wagonjwa wa Covid-19 nchini. Hata hivyo, hakutaja takwimu za mwenendo wa ugonjwa huo.
“Kwa maana hiyo kama wilaya au mkoa, tuone sasa tumejipanga vipi kukabiliana na janga hilo kubwa linaloitesa dunia nzima,” amesema Dk. Gwajima.
Dk. Gwajima amesema wizara yake itaandaa rejesta, itakayoonesha taarifa za halmashauri nchini, kuhusu jitihada ilizochukua kukabiliana na janga hilo.
” Sasa natoa maelekezo kuanzia Jumatatu wizara tutakuwa na rejesta, itakayo onyesha kila halmashauri imefanya vipindi vingapi, hasa kwenye vyombo vyetu vya habari vya ndani vya kuelimisha wananchi kujikinga,” amesema Dk. Gwajima na kuongeza:
“Kwa kunawa mikono , kuvaa barako na tuepuke mikusanyiko isiyo ya lazima.”
Mheshimiwa Dokta umesahau haraka jinsi ulivyokuwa ukitabiri utumiaji wa malimau na tangawizi? Leo vipi umepiga abautani? UNAFIKI