MGOMBEA urais wa Uchaguzi Mkuu wa Kenya kupitia Muungano wa Azimio, Raila Odinga anatarajiwa kumtaja mgombea mwenza leo katika mkutano wa hadhara utakaofanyika katika uwanja wa Kamkunji jijini Nairobi nchini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu (endelea).
Duru za habari kutoka jopo la uteuzi zinasema kiongozi wa chama cha Narc Kenya, Martha Karua amepewa kipaumbele huku kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka na aliyekuwa Mbunge wa Gatanga, Peter Kenneth nao pia wakipendekezwa kwa Raila.
Jopo hilo pia liliwahoji magavana Charity Ngilu (Kitui), Hassan Joho (Mombasa), Lee Kinyanjui (Nakuru) na Wycliffe Oparanya (Kakamega) kuwania nafasi ya mgombea mwenza.
Wengine ni Mwakilishi wa Wanawake wa Murang’a Sabina Chege, Waziri wa Kilimo Peter Munya na aliyekuwa Mbunge wa Emgwen Stephen Tarus.
Jopo hilo lilikuwa likiwakadiria wagombea hao kwa kuzingatia sifa za kikatiba, uelewa wa serikali, utu, ujuzi wa kisiasa, utangamano na uaminifu kwa mgombea urais wa Azimio.
Alama hizo pia zilitolewa kutokana na umuhimu wa kimkakati wa watahiniwa na maoni yao kuhusu vita dhidi ya ufisadi na ukosefu wa ajira kwa vijana.
“Uamuzi wa mwisho ulifikiwa kwa wastani wa mchango wa mtu binafsi wa kila jopo,” Mwenyekiti wa jopo Dk. Noah Wekesa alisema.
Mwenyekiti wa ODM kaunti ya Nairobi, George Aladwa alithibitisha kuwa bosi huyo wa ODM ataongoza viongozi na wafuasi wa Azimio katika mkutano mkubwa Kamkunji, Nairobi.
Hata hivyo, alisema mkutano huo ni wa kuzindua safu ya Azimio ya Nairobi, lakini walio katika karibu na Raila walisema atatumia fursa hiyo kumtaja naibu wake.
“Kutakuwa na mkutano wa hadhara Kamkunji kwa ajili ya viongozi wa Nairobi kutaja wagombeaji wa Azimio Nairobi,” Mbunge huyo wa Makadara aliwaeleza waandishi wa habari nchini humo.
Aidha, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya imesema hadi kufikia Jumanne wiki ijayo, wagombea urais wanatakiwa kuwasilisha majina ya wagombea wenza wao ili waapishiwe.
Leave a comment