HATIMAYE mpeperusha bendera wa Muungano wa Azimio la Umoja-katika Uchaguzi Mkuu nchini Kenya, Raila Odinga amemtangaza Martha Karua kama mgombea mwenza wake. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Raila aamemtangaza mgombea mwenza huyo leoi tarehe 16 Mei, 2022 mbele ya maelfu ya wafuasi wake waliokuwa wamejumuika nje ya ukumbi wa KICC.
Odinga alianza kwa kusoma majina 11 ya viongozi waliowasilisha ombi la kukabidhiwa wadhifa wa mgombea mwenza wake. Baadae aliendelea kusoma historia ndefu ya kazi muhimu ambazo Karua amewahi kufanyia taifa la Kenya.
“Baada ya kushauriana kwa kina tulikubaliana kuwa atakayeshikilia wadhifa wa naibu rais ni sharti awe mwanamke.
“Kwa mara ya kwanza katika historia ya Kenya historia inatuita tuangazia haki za wanawake. Kwa heshima kubwa ningetaka kutangaza mgombea wangu na waziri wa masuala ya haki na katiba, Martha Wangari Karua,” Odinga amesema.
Karua alikuwa amependekezwa na maelfu ya Wakenya pamoja na kundi kubwa la viongozi kuwa mgombea mwenza wa kinara huyo wa ODM katika kinyanganyiro cha Agosti 9.
Odinga amesema alihitaji naibu ambaye atashirikiana naye katika kazi za serikali na sio kushindana naye.
Jumapili wiki iliyopita wazee kutoka jamii ya Kikuyu walimpendekeza kiongozi huyo wa Narc Kenya kuwa mgombea mwenza wa Odinga.
Jopo la kuteua mgombea mwenza wa Azimio pia liliwahoji magavana Charity Ngilu (Kitui), Hassan Joho (Mombasa), Lee Kinyanjui (Nakuru) na Wycliffe Oparanya (Kakamega) na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka.
Wengine ni pamoja na Mwakilishi wa Wanawake wa Murang’a Sabina Chege, Waziri wa Kilimo Peter Munya na aliyekuwa Mbunge wa Emgwen Stephen Tarus.
Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na mwenzake wa KANU Gideon Moi walisusia mkutano huo wa KICC na badala yake kuandaa mkutano mbadala katika ofisi za SKM Command Centre mtaani Karen.
Kalonzo alipewa wadhifa wa mkuu wa mawaziri katika serikali ambayo Odinga anakusudia kuunda.
Leave a comment