MAWAKILI wanaomwakilisha Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi nchini (TSNP), Abdul Nondo wamefungulia kesi Mkuu wa jeshi la Polisi nchini (IGP), Mkurugenzi wa Upelelezi wa makosa ya Jinai (DCI), Mwasheria Mkuu wa Serikali (AG), kwa kumshikilia kwa zaidi ya saa 48 mwanafunzi huyo. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Nondo alitoweka jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia Machi 8, mwaka huu kabla ya kupatikana wilayani Mafinga, Iringa ambapo alidai kuzinduka na kujikuta eneo hilo baada ya kutekwa na watu wasiofahamika. Hata hibyo taarifa ya Jeshi la Polisi imedai kuwa kijana huyo hakutekwa bali alienda mkoani humo kumtembelea mpenzi wake.
Tangu tarehe 8 Machi mwaka huu, polisi wanamshikilia mwanafunzi huyo, ikiwa ni zaidi ya siku 11 sasa. Awali alisafirishwa kutoka Iringa mpaka Dar lakini haijajulikana amehifadhiwa katika kituo gani cha polisi huku mawakili na ndugu zake wakidai kuzuiwa kumuona kwa kipindi hicho chote.
Mawakili wa mtandao huo wakiongozwa na Jebra Kambole, Jones Sendodo na Reginald Martine wamefungua shauri la kumtaka IGP, AG na DCI wajieleze kwanini wanaendelea kumshikilia Nondo, na kisha wamuachie kwa dhamana kijana huyo au wamfikishe mahakamani haraka, hilo kwenye mahakama Kuu kanda ya Dar es Salaam kushinikiza kufikishwa mahakamani kwa Nondo.
Wakili Jones Sendodo ameiambia MwanaHALISI Online ameeleza kuwa kesi hiyo imeshafunguliwa na imepangiwa Jaji na kwamba itasikilizwa Tarehe 21 Machi.
Wito umetolewa leo Mahakama kuu mbele ya Jaji SAMEJI kwamba DCI,IGP na AG wanapaswa kufika mahakamani 21/03/2018 kujibu kesi ya Abdul Nondo @MariaSTsehai @zittokabwe @CarolNdosi @JamiiForums @MwananchiNews @may_tash17 @halimamdee @godbless_lema @Ishabakaki @Chahali @Udadisi
— Jebra Kambole (@Advocate_Jebra) March 19, 2018
Wakili Sendodo amesema kuwa Jeshi la Polisi linatakiwa limmpeleke mahakamani Nondo ili kumshtaki kwa mashtaka wanayoyadai au wamuachie kwa dhamana ya polisi kama bado hawajakamilisha upelelezi.
“Polisi wanaendelea kumshikilia ilihali sisi mawakili wake hawaturuhusu tumuone.”
Kamanda wa Polisi Kanda maalumu ya Dar es Salaam Lazaro Mambasasa aliripotiwa hivi karibuni akisema kuwa bado wanaendelea na upelelezi kwenye kesi hiyo na kwamba watamfikisha mahakamani upelelezi ukikamilika.
Leave a comment