BENKI ya NMB imetoa msaada wa vifaa vya elimu katika shule tano za halmashauri ya wilaya ya Kilosa na Mvomero vikiwa na thamani ya sh35milioni ikiwa sehemu ya kupunguza changamoto za elimu mkoani Morogoro. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Vifaa vilivyotolewa ni pamoja na mabati, mbao, misumari na madawati kwa shule za sekondari Murrad Sadiq Sekondari, Mziha Sekondari huku kwa shule za msingi ni Madizini, Mlali, Matongolo na Mkwatani.
Wakizungumza wakati wa hafla iliyofanyika katika shule hizo kwa nyakati tofauti, Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Matongolo wilaya ya Kilosa, Sifa Jonas alisema shule hiyo imepokea msaada wa madawati 50 yenye thamani ya sh5milioni ambayo yatasaidia tatizo la wanafunzi kukaa chini wakati wa masomo yao ya kila siku.
Sifa alisema shule ya msingi Matongolo ina jumla ya wanafunzi 2379 wavulana wakiwa 1155 na wasichana 1224 huku kukiwa na madawati 236 huku kukiwa kukihitajika madawati 557.
“Msaada huu wa NMB wa kutukabidhi madawati 50 utasaidia kupunguza adha ya wanafunzi kukaa chini kwani mpaka sasa tuna upungufu wa madawati 557 na madawati yaliyopo ni 236 ambayo hayakidhi mahitaji kwa wanafunzi 2379 wanaosoma shule yetu.
“Hivyo bado kunahitaji nguvu za ziada kupata madawati 557 ili watoto wasiendelee kukaa chini wakati wa masomo yao,” alisema Mwalimu Mkuu Sifa.
Shule ya sekondari Murrad Sadiq Mvomero na shule ya sekondari Mziha zimepokea vifaa vya kuezekea majengo ya vyumba vya madarasa kila mmoja vifaa vya thamani ya sh5milioni ili kukabiliana na wimbi la wanafunzi wataojiunga na kidato cha kwanza Januari mwaka 2023 .alisema Afisa Elimu Msingi wilaya ya Mvomero, Bruno Sangwe.
Mwanafunzi wa darasa la tano shule ya msingi Madizini wilaya ya Mvomero, Najma Ally amesema shule yao inakabiliwa na changamoto ya wanafunzi wengi kukaa chini na msaada huo wa madawati 52 vitasaidia kupunguza changamoto ya wao kukaa chini
Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Kati, Nsolo Mlozi alisema benki hiyo kwa mwaka huu imetenga kiasi cha zaidi ya sh. Bilioni mbili kwa ajili ya kusaidiana na serikali kutatua changamoto katika sekta ya elimu, Afya na yanapotokea majanga.
Leave a comment