BENKI ya NMB nchini Tanzania imezindua huduma maalumu ya kuweka na kutoa fedha kirahisi kupitia wakala watakao tumia simu zao za mkononi tu. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Huduma hiyo ya NMB Pesa Wakala imezinduliwa jijini Dar es Salaam, Jumatatu tarehe 28 Machi 2022, ikilenga kusogeza ‘Karibu Zaidi’ huduma za kifedha kwa wananchi.
Aidha, huduma hiyo itatoa fursa za ajira kwa Watanzania, lengo likiwa kuongeza idadi ya mawakala kutoka 11,000 wa sasa hadi 100,000 miaka mitano ijayo.
Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alivitaja vigezo vya mtu kuomba uwakala wa NMB Pesa Wakala ni pamoja na Leseni ya Biashara, Kitambulisho cha Taifa (NIDA) na simu ya mkononi ya aina yoyote (smartphone au kitochi).
“Tunaahidi kwamba kupitia teknolojia hii mpya na ya aina yake, mfanyabiashara mwenye vigezo vilivyotajwa, ataweza kuomba na kuwa ‘activated’ ndani ya masaa 48 tu toka atakapoomba matawini kwetu kote nchini, naye ataweza kuhudumia wateja wake,” alisema Mponzi.
“NMB ni vinara wa huduma suluhishi zinazowafanya Watanzania wafurahie huduma za kibenki. Tunafanya hivyo kwa sababu sisi ni benki inayotegemewa na Watanzania wote, ndio maana tunayo furaha kuzindua NMB Pesa Wakala ili kuharakisha maendeleo ya Sekta ya Fedha nchini,” alisema Mponzi.
Afisa huyo alisema, huduma hiyo itaenda sambamba na ile ya vituo vya mauzo (PoS) na kwamba tofauti huitaji kupata mashine maalumu na sasa mteja anaweza kutoa huduma hii kupitia simu yake ya mkononi tu, bila kuhangaika kupata mashine za PoS ambazo zinatumia kadi.
“Hii ina maana kwamba wanaotaka uwakala itakuwa rahisi zaidi kwao kwa kutumia simu zao. Ukihitaji kuwa wakala, unahitaji kuwa na simu aina yoyote, leseni ya biashara, kitambulisho cha NIDA na kwa mtindo huu kupata uwakala huu ni rahisi.”
“Tunaamini NMB Pesa Wakala itaharakisha kusambaza mawakala wengi zaidi wa kusogeza huduma kwa jamii, lakini pia itakuwa fursa ya kuongeza ajira miongoni mwa Watanzania,” alisema.
“Tunajisikia fahari kuja na suluhishi hii na tuna kazi kubwa ya kufanya kuhakikisha tunaendelea kuwa vinara wa huduma za kifedha nchini,” alisisitiza Mponzi.
Aliwataka Watanzania kuendelea kuwa wateja wa NMB na kwamba wenye leseni za biashara, vitambulisho vya NIDA, wajitokeze kuomba uwakala kwenye matawi yaliyo jirani yao, ili kuwa sehemu ya familia ya NMB, iliyoshinda Tuzo ya Benki Salama Zaidi Tanzania 2021.
Leave a comment