WATANZANIA wameshauriwa kujiunga na huduma za benki ili kuwawezesha kupata mikopo ambayo itawasaidia kufanya shughuli za ujasiliamali kwa lengo la kujikwamua kiuchumi, anaandika Moses Mseti.
Ushauri huo umetolewa leo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella na Kaimu Afisa Mkuu wa wateja wadogo na wakati kutoka Benki ya NMB, Abdul Nsekela wakati wa ufunguzi wa tawi la benki hiyo katika barabara ya Pamba Jijini Mwanza.
Lengo la benki hiyo kufungua tawi hilo ni kuwasogezea huduma wananchi ili kuwasaidia kutunza fedha na wale ambao wanahitaji mikopo na huduma mbalimbali za benki waweze kupata huduma kiurahisi.
“Wananchi wanapaswa kutambua huduma za benki ni muhimu kwa ustawi wa jamii kwa maendeleo ya kiuchumi na pia watu kujikwamua katika wimbi la ukosekanaji wa mitaji ya kuendeshea shughuli za kibiashara.
Nsekela alisema, NMB kwa kanda ya ziwa ina matawi 32 ya benki yanayofanya idadi kamili ya matawi katika nchi zima kufikia zaidi 210, mawakala 241 jijini Mwanza na kwamba wamebuni bidhaa bora na nafuu ambayo ni akaunti ya chap chap ambayo mpaka sasa imeisha wafikia wananchi wengi wanaonufaika na maendeleo ya sayansi na teknolojia,pamoja na akaunti ya Fanikiwa ambayo ni mahususi kwa wajasiriamali.
Ofisa Mkuu wa Mauzo, Tom Bogols alisema NMB kwa kutumia faida zinazopatikana katika shughuli za benki imenunua vitanda 11 vya wagonjwa pamoja na mashuka ambavyo vitakabidhiwa katika hospitali ya wilaya ya Nyamagana vilivyogharimu Sh. Milioni 10, ili kupunguza changamoto ya ukosekanaji wa miundombinu hiyo.
Mkuu wa mkoa huo, Jonh Mongella aliwataka wananchi wa mkoa wa Mwanza kuchangamkia fursa iliyowafikia katika maeneo yao ili kujikwamua katika masuala muhimu ya kijamii huku akisema serikali inatambua mchango wa benki hiyo.
“Serekali inatambua juhudi zenu za kuwawezesha wananchi kupata mikopo ya wafanyakazi, wakulima na wafanyabiashara na ndiyo maana serikali ya awamu ya tano imeweka mikakati mizuri ya kupunguza umaskini kwa wananchi wake,” alisema Mongella.
Leave a comment