WANAHISA wa Benki ya NMB wameidhinisha gawio la Sh 143.1 bilioni kwa mwaka 2022, sawa na Sh 286 kwa kila hisa moja katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa 23 wa Wanahisa uliofanyika kwa njia ya mtandao leo Ijumaa. Hili ni ongezeko la 48% ukilinganisha na gawio la jumla la Sh 96.7 bilioni ililolipwa mwaka 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Benki hiyo ikiwa inaandika historia ya kutimiza miaka 25 ya kuwahudumia watanzania, hili ni gawio kubwa zaidi kuwahi kutolewa na taasisi ya fedha nchini kwa wanahisa wake. Gawio hilo litalipwa kufikia tarehe 14 Juni 2023.
Akizungumza katika mkutano mkuu wa wanahisa uliofanyika kwa njia ya mtandao, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna amesema miaka minne iliyopita, walilipa gawio la Sh 33 bilioni kwa wanahisa wao lakini kwa mwaka 2022 gawio limeongezeka na kufikia Sh 143.1 bilioni.
Amesema ongezeko hilo la gawio linaendana na ongezeko la mchango NMB katika uchumi wa Taifa na maendeleo ya wananchi kupitia programu yetu ya uwajibikaji kwa jamii.
“Kwa mwaka huu tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 6.2 zinazoelekezwa kwenye sekta ya afya, elimu, mazingira, elimu ya fedha na usaidizi wa majanga.
“Mafanikio ya Benki yetu ni matokeo ya mazingira mazuri ya kibiashara yaliowekwa na Serikali yetu, Imani ya wanahisa na wateja wetu, juhudi za wafanyakazi wetu, usimamizi mzuri wa Benki Kuu ya Tanzania na ushirikiano mzuri uliopo na wadau wetu wote. Tunawashukuru na tuendelee kuwa pamoja katika safari yetu ya mafanikio,” amesisitiza Zaipuna.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya NMB, Dkt. Edwin Mhede amesema: “Bodi yetu itaendelea kuwa ya kibunifu na kusimamia ukuaji wa Benki ili kuhakikisha wanahisa wetu wanaendelea kunufaika na uwekezaji wao.
“Bodi ina imani kubwa na mikakati iliyopo na imedhamiria kuhakikisha NMB inaendelea kuwa Benki kiongozi nchini na inakuwa na mchango mkubwa zaidi wa kiuchumi na kijamii,” amesema.
Leave a comment