WIZARA ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi ya Zanzibar imeipongeza Benki ya NMB kwa kuleta masuluhisho maalum yalio rafiki kwa ajili ya wakandarasi huku ikiamini ndio njia rahisi ya kusaidia kuwakuza wakandarasi wazawa kiuchumi. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamesemwa na Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk. Khalid Salum Mohammed alipokuwa anazindua rasmi warsha ya Benki ya NMB pamoja na wakandarasi wa Zanzibar ikiwa na lengo la kuwatambulishia suluhisho mpya kwaajili ya wakandarasi.
“Tuna kila sababu ya kuupongeza uongozi mzima wa Benki ya NMB kwa kuamua kuja na suluhisho ambalo linawalenga wakandarasi, hili ni jambo jema na naamini litawaongezea ari ya kufanya kazi kwa weledi na ubora na kuinua wakandarasi wazawa,” alisema Dk. Khalid.
Mbali na kuwasihi wakandarasi kuchangamkia fursa hizo zinazoletwa na benki ya NMB, Waziri huyo aliwasihi wakandarasi kutumia fedha za mikopo wanaopata kutoka kwa mabenki kwaajili ya kazi waliokopea na sio kwa shuguli zingine kwa inaweza wapa ugumu katika kurejesha mkopo huo.
“Tusiwe na tabia ya kubadili matumizi ya mikopo tunayo pewa kwani kwa kufanya hivyo, italeta ugumu katika kurejesha mkopo huo na baadae badala ya kunyayuka kama ilivyo adhma ya NMB basi tutaishia kushuka chini zaidi. Matumizi mazuri ya fedha ni jambo la muhimu na la kuwa nalo makini katika kutekeleza kazi zetu haswa kwa fedha za mikopo tunazochukua kutoka kwa Mabenki kama NMB,” alisema Dk. Khalid.
Akizungumza katika warsha hiyo, mwakilishi wa Benki ya NMB ambae ni Mkuu wa Idara ya Miamala wa Benki hiyo, Linda Teggisa alisema benki hiyo imesimama katika nafasi ya kuendelea kuongeza fursa ya upatikanaji wa huduma za kifedha ili kuendelea kuwawezesha wakandarasi kutekeleza miradi mbalimbali.
“Benki ya NMB ni mdau mkubwa wa sekta ya ujenzi nchini hivyo imeona umuhimu wa kuandaa warsha hii na kuwakutanisha wadau wote wa sekta hiyo kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kuwaelezea fursa nyingi kutoka Benki ya NMB ambapo tunaamini baada ya hapo, zitakwenda kuongeza tija katika ufanyaji kazi wa makandarasi hawa,” alisema Linda Teggisa.
“Benki yetu imejikita pia katika kutoa huduma za dhamana za zabuni kwajili ya miradi au manunuzi (unsecured bid bond) pamoja na dhamana za utekelezaji (performance guarantee) au dhamana za malipo ya awali (advance payment guarantee). Zote ambazo hatuhitaji Dhamana,” aliongeza mkuu huyo wa Idara ya Miamala.
Akizungumza kwa Niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibu, Mkuu wa wilaya ya Mjini, Rashid Simai Msaraka alisema sekta ya ujenzi imekuwa ni sekta ya muhimu sana kwa Zanzibar kwa sasa kwani ni miongoni mwa Sekta ambazo zinaongeza ajira zilizo rasmi na zisizo rasmi kwa wananchi wa Zanzibar.
“Sekta ya Utalii na ujenzi ndio sekta zilizoongeza ajira nyingi sana kwa Zanzibar kwa kipindi hiki cha Karibuni, zaidi ya ajira 50,000 zimetokana na sekta hizi huku sekta ya Ujenzi ikichangia ajira mpya 26,371.
“Hili ni jambo ambalo ambalo linastahili pongezi kwa sekta hii na tunapoona taasis za fedha zinaamua kuongeza nguvu kwa sekta basi tunapata mwanga kuwa sio tu kuwanyayua wakandarasi lakini linaenda kupunguza changamoto ya upatikanaji wa Ajira kwa Zanzibar,” alisema Msaraka.
Leave a comment