BENKI ya NMB imeibuka kidedea katika taasisi za kibenki na kifedha kwenye maonesho ya Nanenane yaliyofanyika kitaifa 2022 mkoani Mbeya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya…(endelea).
Mbali na kunyakua tuzo hiyo ya kitaifa, benki hiyo pia iliibuka mshindi katika maonesho ya kanda yaliyofanyika kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Kanda ya Ziwa na Kanda ya Kaskazini,
Akizungumza muda mfupi baada ya kupokea cheti cha ushindi, Mkuu wa idara ya Kilimo Biashara wa Benki ya NMB, Isaac Masusu alisema tuzo hizo zinasisitiza dhamira ya benki hiyo kutoa huduma za kibenki zisizo na kifani zinazokidhi mahitaji ya wateja wake.
Masusu wakati wa hafla hiyo alisisitiza dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kutoa bidhaa zinazoendana na matakwa ya wateja.
Alisema benki yake itaendelea kufanya kazi na wadau mbali mbali kuongeza mnyororo wa thamani wa sekta ya kilimo na kuongeza kuwa benki hiyo tayari imeshusha kiwango cha riba mpaka tarakimu moja kwa wateja wa benki hiyo katika sekta ya kilimo.
“Sisi kama benki, tunaelewa kuwa sekta ya kilimo ina mchango mkubwa katika uchumi na tutaendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wote kusaidia maendeleo ya sekta hii,” alisema.
Akizungumzia cheti cha ushindi wa benki, Masusu alisema, “napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru wafanyakazi wenzangu wote waliofanya kazi bila kuchoka kuhakikisha kuwa tunasimama kidete katika maonyesho ya Nane Nane. Pia ningependa kuchukua fursa hii kuushukuru uongozi wa benki ya NMBa kwa miongozo na Usimamizi wake wa karibu.”
Maonesho ya Nane Nane yaliyowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo yalizinduliwa na Makamu wa Rais, Dk Philip Mpango Agosti 1, 2022 na kufungwa rasmi na Rais Samia Suluhu Hassan Jumatatu hii Agosti 8, 2022.
Leave a comment