KWA kutambua umuhimu wa sekta ya michezo nchini, Benki ya NMB imeingia makubaliano na timu ya Yanga SC. na kuwa benki ya kwanza nchini kuwawezesha mashabiki na wanachama wa Yanga kupata kadi za uanachama kupitia matawi yote ya NMB yaliyoenea nchi nzima. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Makubaliano haya yamesainiwa leo tarehe 1 Julai 2023 jijini Dar es Salaam na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara NMB, Filbert Mponzi na Rais wa Klabu ya Yanga, Eng. Hersi Said na kushuhudiwa na viongozi wengine wa Benki na Klabu.
Akizungumza baada ya kusaini makubaliano hayo, Mponzi amesema hatua hiyo ni mwendelezo wa ubunifu wa Benki hiyo katika kuboresha huduma zake nchini.
Amesema kwa kuwa benki hiyo inayomatawi nchi nzima, itakuwa rahisi kwa wapenzi na wafuasi wa Yanga Sc. kujisajili kupitia matawi ya NMB.
Aidha, amesema watakaojisajili na kupatiwa kadi za uanachama, watafaidika kwa namna mbalimbali ikiwamo kutumia kadi hizo kufanya miamala ya kibenki ndani ya nje ya nchi hasa ikizingatiwa kadi hizo zinatambulika kimataifa “master card”.
Mponzi ameongeza kuwa kupitia matawi 900 ya klabu ya Yanga nchi nzima, NMB itaanzisha mpango wa kuyawezesha matawi hayo kujiendesha kibiashara na kuwa mawakala wa NMB.
Amesema mbali na huduma za uanachama, NMB itaanzisha Bima ya Mwananchi ambayo itakua na gharama nafuu.
Aidha, akifafanua huduma zitakazopatikana kutokana na makubaliano hayo, Rais wa Yanga amesema wanachama wa Yanga wataweza kutumia mtandao mpana wa NMB unaojumuisha matawi zaidi ya 228 kote nchini kufanya usajili wa wanachama na mashabiki wa Yanga, wakiwemo wenye umri chini ya miaka 18. Kadi hizi maalum zitakua na nembo za Yanga na NMB.
Amesema mwanachama wa Yanga atalipia Sh. 34,000 kama kianzio cha kupata kadi ya Yanga (Sh 5,000 ni malipo ya kadi, 5,000 amana ya kuanzia na Sh 24,000 ni ada ya Mwanachama kwa mwaka mzima).
“Kadi za mashabiki ambao sio wanachama – Malipo yatakua Sh 22,000 tu (Sh 5,000 ni ya kadi, 5,000 amana ya kuanzia na Sh 12,000 ni ada ya shabiki kwa mwaka mzima).
“Kadi hizi hazitakua za uanachama/ushabiki tu, pia zina uwezo wa kufanya kazi kama kadi ya Benki! Unaweza kufanya miamala yote ya kibenki ikiwemo kuiwekea pesa, kutoa hela katika ATM na kufanya malipo mtandaoni na katika vituo vya malipo (POS).
“Wanachama wanaweza kupata kadi za Malipo ya Kabla (Prepaid Card) ambayo huitaji kuwa na akaunti nasi na kufanya malipo kwa kupitia mtandao au kwenye Point of Sales (POS).
“Wanachama na mashabiki watanufaika na huduma na ofa mbalimbali za NMB ikiwemo mikopo isiyokua na dhamana (Mshiko Fasta) na punguzo la bei wakifanya malipo kupitia NMB Lipa Mkononi (QR),” amesema.
Amesema usajili huu utaanza rasmi tarehe 10 Julai 2023 kwenye matawi yote ya NMB hivyo wapenzi na wafuasi wa klabu hiyo watapaswa kutembelea matawi ya Benki hiyo ili kujisajili.
Leave a comment