KATIKA kuhakikisha inaunga mkono juhudi za serikali za kuboresha huduma za jamii kwa wananchi wake, Benki ya NMB imetoa vifaa mbalimbali kwenye shule za msingi, sekondari vya thamani ya Sh.150 milioni kwa mikoa ya Mbeya, Kilimanjaro na Singida. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Vifaa hivyo vimetolewa kwa nyakati tofauti mwishoni mwa wiki iliyopita, ambapo mkoa wa Mbeya imepata vifaa vya thamani ya Sh.70 milioni hafla ambayo ilihudhuriwa na Spika wa Bunge la Tanzania, Dk.Tulia Ackson.
Afisa Mkuu Wateja Binafsi na Biashara wa benki hiyo, Filbert Mponzi wakati wa kukabidhi vifaa hivyo kwa shule za Sekondari za Itgano, Itende na Iduda yenye kidato cha tano na sita pamoja na za Msingi Inyala na Ikuti za jjini Mbeya.
Alisema benki hiyo imetoa vifaa kwenye shule hizo ambavyo ni mabati 200 na madawati 100 kwa kila shule vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya Sh 70 milioni.
Alisema NMB itaendelea kushirikiana na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuboresha sekta ya elimu nchini ili kuwasaidia wanafunzi kusoma katika mazingira mazuri.
Naye Spika wa Bunge, Dk Tulia alipongeza NMB kwa mchango wake katika sekta ya elimu huku akieleza msaada huo utaenda kumaliza tatizo la bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Iduda.
“Tunazo shule tano ambazo zitanufaika na msaada huu, tunaamini lile bweni la wasichana hapa Iduda linaenda kuezekwa, wanafunzi nao wakisoma kwenye madawati mazuri,” amesema Dk Tulia.
Mkoani Singida Benki hiyo ilitoa vitanda 80 kwa ajili ya wanafunzi wa bweni shule za Sekondari Tumaini na Lulumba zote za Wilayani Iramba pamoja na madawati 100 kwa shule za msingi Ipuli na Ikungu zote za halmashauri wa Wilaya Mkalama.
Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Kati, Nsolo Mlozi alisema vifaa hivyo vimegharimu kiasi cha Sh.31 milioni huku akibainisha vitanda vilivyotolewa vitakuwa na uwezo wa kutumiwa na wanafunzi 160 huku kila shule ikiwa pata madawati 50.
Nsolo alisema msaada huo uliotolewa na NMB unatokana na faida iliyoipata kwa hiyo wanarudisha kwenye jamii sehemu ya faida hiyo kupitia misaada mbalimbali inayotolewa na benki hiyo kwa baadhi ya maeneo nchini.
Mkuu wa Wiliya ya Iramba, Selemani Mwenda akizungumza baada ya kupokea msaada wa vitanda kwa ajili ya shule hizo mbili aliwashukuru NMB kwa msaada huo na kuahidi kuwa utakuwa chachu ya shule hizo kuendelea kufanya vizuri katika masomo yao.
“Shule yetu hii ya Lulumba imekuwa ikifanya vizuri katika matokeo ya mitihani ya Kitaifa na imekuwa ikiongoza kwa matokeo katika Mkoa wetu kwa kushika nafasi ya kwanza na imekuwa ikishika nafasi ya juu Kitaifa hivyo vitanda hivi tulivyokabidhiwa leo itakuwa chachu ya kufanya vizuri zaidi,” alisema.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, Sophia Kizigo akashukuru NMB kwa msaada wa madawati, huku akizuomba taasisi nyingine kuiga mfano wa benki hiyo katika kuunga mkono juhudi za serikali kuwaletea wananchi wake maendeleo.
Mkoani Kilimanjaro Benki hiyi imetoa viti pamoja na meza 200 kwa shule ya Sekondari Kivisini iliyopo katika Wilaya ya Mwanga, ambapo vifaa hivyo vilipokelewa na Mkuu wa Wilaya hiyo Abdala Mwaipaya.
Meneja wa NMB Kanda a Kaskazini, Dismas Prosper akikabidhi viti na meza hivyo alisema kuwa vimegharimu kiasi cha Sh.20.8 milioni na kubainisha kuwa lengo la kutolewa kwa vifaa hivyo ni kuhakikisha wanafunzi wanasoma katika mazingira bora.
Leave a comment