MKUU wa Mkoa wa Dodoma (RC), Anthony Mtaka ameagiza Jiji la Dodoma kuharakisha sheria ndogondogo za mazingira ili kuweka hali ya usafi katikati ya Jiji hilo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Mtaka ametoa agizo hilo kwa Naibu Meya wa Jiji la Dodoma, Emmanuel Chibago wakati wa kupokea vifaa vya kuhifadhia taka vilivyotolewa na Benki ya NMB ili kusaidia utunzaji wa mazingira.
NMB wamekabidhi mapipa 100 yenye thamani ya zaidi ya Sh20 milioni wakiahidi kuendeleza ushirikiano na mkoa ili kuweka mji katika hali ya usafi.
RC Mtaka amesema mapema mwaka huu Jiji hilo walitembelewa na Makamu wa Rais, Dk Philip Mpango kwa ajili ya kukagua usafi lakini hakuridhishwa na usafi.
“Siku ile tulipata aibu kubwa, niliamua kuandika kwa mkono wangu kuomba vifaa hivi kwa Benki ya NMB na leo wameleta, Sasa naagiza vikabidhiwe kwa maandishi ili kila mmoja awe na wajibu wa kutunza na kuvifanyia kazi,” amesema Mtaka.
Amesema bila kuwa na sheria za kuwajibishana bado Dodoma itaendelea kuwa na hali ya uchafu ambayo ni aibu kwa watu wote.
Awali, Afisa Mkuu wa Feedha wa NMB, Juma Kimori amesema makabidhiano ya vifaa hivyo ni mipango ya benki hiyo katika kurudisha sehemu ya faida kwa wananchi baada ya kodi ambapo mwaka huu wametenga Sh2.8 bilioni ikiwa na ongezeko ukilinganisha na Sh2 bilioni za mwaka jana.
Kimori amesema walipokea ombi la vifaa vya kutunzia taka (dusty been) 350 kutoka kwa Mkuu wa Mkoa lakini kwa kuanza wametoa 100.
Hata hivyo, mara baada ya maelezo ya Mkuu wa Mkoa, Kimori ametangaza kuwa ndani ya siku mbili benki itakabidhi mapipa mengine 50 na hivyo kufanya thamani halisi ya vifaa hivyo kuwa Sh30 milioni.
Amewataka wananchi kuendelea kuwekeza katika banki hiyo ambayo imerahisisha huduma zake ikiwemo mikopo ya haraka kwa wajasiliamali ambayo inatolewa kwa njia ya simu bila kujaza fomu.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa huo, Dk Fatuma Mganga amesema baada ya makabidhiano hayo, sheria za usafi zitaanza kutekelezwa kwa mtu atakayetupa taka hovyo.
Dk Mganga amesema awali ilikuwa ngumu kutekeleza sheria hiyo kwa sababu maeneo mengi hayakuwa na vifaa vya kuhifadhia taka hivyo kila mmoja alitupa kama anavyoona inafaa.
Ameema licha ya juhudi kubwa za usafi lakini maeneo ya wapi watupe taka ilikuwa ni changamoto kubwa hivyo kufanya wakati mwingine sheria zifumbiwe macho.
Leave a comment