BENKI ya NMB imeanzisha huduma maalum kwa wateja wao kujiwekea akiba kila wanapofanya mialama. Anaipoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Huduma hiyo ya kwanza nchini, inajulikana “Spend to save”- miamala yako ni akiba yako, imezinduliwa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na maofisa waandamizi wa benki hiyo.
Aidha, huduma hiyo yenye lengo la kuwahamasisha wanancji kujiwekea akiba, ni kwa ajili ya akaunti binafsi, akaunti za chap chap na akaunti za mwanachuo.
Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara, Filbert Mponzi, alisema “Spend to Save” inadhihirisha ubunifu wa hali ya juu wa benki hiyo na uongozi wake wa kuanzisha suluhisho wezeshi za kibenki.
Alisema, huduma ya “Spend and Save” inapatikana kwa mteja kujisajili kupitia zaidi ya ATM 8,000 za benki hiyo zilizosambaa nchi nzima na kuweka malengo kwa asilimia ya kila muamala anaoufanya.
Mponzi alisema, kiasi kitakachokatwa kwa ajili ya akiba ni kati ya asilimia mbili hadi kumi ya kila muamala utakaofanyika na miamala itakayohusika ni ile inayofanywa kupitia ATM, POS, NMB Direct au NMB Mkononi.
“Hili ni jambo kubwa kipindi hiki tunapowakumbusha Watanzania na wateja wa NMB kujitunzia akiba kwa maisha ya baadae,” alisema Mponzi.
“Huduma hii ni ya kwanza na ya aina yake kuwahi kutokea nchini Tanzania ambapo mteja anajitunzia fedha zake kupitia miamala yake anayoifanya iwe kununua kitu, kutoa fedha kutoka kwenye akaunti yake au hata kutuma fedha,” alisema.
Mponzi alisema, benki hiyo imeanzisha utaratibu huo baada ya kugundua wateja wake wengi hawana tabia ya kuweka akiba na hivyo kuona umuhimu wa kuwaletea huduma ambayo itawasaidia kuweka akiba mara kwa mara na kwa malengo.
Aidha, uzuri wa huduma hiyo ni mteja kuweza kutoa fedha zake kutoka kwenye waleti na kuzirudisha kwenye akaunti muda wowote na atakapofanya hivyo ataruhusiwa kutoa mpaka asilimia 50 ya fedha iliyohifadhiwa.
Pia, mteja anaweza kujitoa kwenye wallet na fedha zilizohifadhiwa zitarudishwa kwenye akaunti mama.
“Huu ni muendelezo wa huduma ambazo NMB tumekuwa tukianzisha ili kusaidia wateja wetu kwa kutoa suluhisho za huduma za kibenki zenye tija hapa nchini na kutufanya kinara wa kufanya hivyo,” alisema Mponzi
Naye Mkuu wa Idara ya Bidhaa, Aloyse Maro, alisema huduma hiyo mpya pia inaongeza namna bora ya kuwahudumia wateja.
Leave a comment