KWA mara nyingine Benki ya NMB nchini Tanzania, katika kuendeleza ubunifu na kuwarahisishia huduma wateja wake, imekuja na mfumo mpya wa malipo ya huduma wa kidijitali utakaotumiwa na watu wa maeneo yote hasa walio masokoni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Kampeni za kuwafikishia ujumbe na huduma hiyo ya kidijitali inayojulikana kama Teleza Kidijitali ilizinduliwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam katika mitaa yenye shughuli nyingi hasa zinazohusu wamachinga.
Aidha, mwishoni mwa wiki NMB ilifikisha mfumo huo mpya wa Teleza Kidigitali jijini Arusha ambapo lengo kuu ni kusogeza huduma kwa wananchi ili waweze kutumia fursa mbalimbali ikiwemo mikopo nafuu.
Akizindua mfumo huo katika Soko la Kilombero jijini Arusha, Afisa Mkuu wa Biashara na Wateja Binafsi wa NMB, Filbert Mponzi alisema mfumo huo wa kipekee ni kampeni ambayo itawafanywa Watanzania wengi kuingia katika mfumo wa kibenki.
“Wafanyabishara wadogo na wateja wao mara nyingi huona uzito kutumia malipo kwa njia ya kibenki, lakini kupitia mfumo huu wa kijanja kila mmoja atakuwa na uwezo wa kuingia katika mfumo wa kibenki wakati wa kufanya miamala, ambapo watafanya shughuli zao kwa njia rahisi na salama,” alisema Mponzi.
Alibainisha kupitia mfumo huo wananchi hawatakuwa na ulazima kufika kwenye matawi ya NMB kufanya miamala yao, lakini pia watakuwa na fursa ya kupata huduma ya Mshiko Fasta ambao ni mkopo wa wateja wadogo na inayopatikana kwa njia ya NMB mkononi.
“Kwa kupitia huduma hii, mteja atafungua akaunti na kutokana na miamala yake anaweza kujipatia mkopo wa Shilingi 100,000 lakini pamoja na hilo tunawaletea NMB pesa wakala ambayo imerahisishwa zaidi,” alisema Mponzi.
Aidha, Mponzi aliwasisitiza wale wenye sehemu zao za biashara Benki ya NMB inatoa huduma ya Lipa Mkononi ambapo inamuwezesha Mfanyabiashara au mjasiriamali kulipwa pesa za mauzo moja kwa moja katika akaunti yake kirahisi na kwa usalama bila kulazimika kuhamisha fedha nyingi kutoka eneo lake la biashara kwenda tawi la benki.
“Lengo kubwa zaidi tunataka wananchi wengi kuingia katika mfumo wa kibenki na kutokana na ukweli kuwa benki ya NMB ni benki iliyofika kila mahali itakuwa na mchango mkubwa sana katika kuhakikisha inawahudumia wananchi wengi zaidi,” alisema Mponzi.
Nao baadhi ya wafanyabiashara wa Soko la Kilombero walisema wanaishukuru benki ya NMB kwa kuwaletea hudumu hiyo itakayowasaidia kupata mikopo ya fedha kwa ajili ya kujiinua kichumi.
“NMB wametuletea njia rahisi ya kufanya biashara, kwa sababu wapo baadhi ya wateja wanataka kununua kwa njia ya kibenki hii itaturahisishia hata hatutakuwa na haja ya kutafuta chenji. Vilevile fedha zetu za mauzo zitakuwa salama hatutakuwa na haja ya kusafirisha fedha nyingi kuzipeleka benki,” alisema Hassan Athumani.
Baadhi ya wachuuzi waliozungumza na mwandishi wetu walieleza imani yao kwa mfumo huu mpya wa kidijitali ambapo walieleza kuwa kila siku NMB inawapa sababu mpya ya kufanya nao biashara kwa kuwa sasa hivi huduma nyingi za kibenki zinafanyika kwa njia ya simu.
Leave a comment