WANACHAMA wa Klabu ya Simba, jijini Dar es Salaam, wamekutana kumchagua Mwenyekiti wa timu hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mkutano huo mkuu wa Simba, unafanyika leo Jumapili, tarehe 7 Februari 2021, Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano ya Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.
Wanaowania nafasi hiyo ni; waliowahi kuwa wabunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Murtaza Mangungu wa Kilwa Kaskazini mkoani Lindi na Juma Nkamia wa Chemba, jijini Dodoma.
Wawili hao kwa pamoja, walishindwa kutetea nafasi zao, ambapo Mangungu alishindwa kwenye uchaguzi mkuu wa 2015 na mgombea wa Chama cha Wananchi (CUF), Vedasto Edga Ngombale, huku Nkamia yeye alishindwa kwenye kura za maoni ndani ya chama chake kwenye jimbo la Nchemba, mkoani Dodoma.
Baada ya kushindwa katika mchakato wa kura za maoni ndani ya CCM na sasa, wanachuana kuongoza mabingwa hao watetezi wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Uchaguzi huo mdogo, unafanyika baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Klabu hiyo, Swedi Nkwabi, kujiuzulu Septemba 2019, baada ya kuwapo kwa mvutano wa hapa na pale wa kiungozi ndani ya timu hiyo.
Baada ya kujiuzulu nafasi hiyo, Simba ilimteua Mjumbe wa Bodi ya Klabi hiyo, Mwina Seif Kaduguda kukaimu nafasi hiyo.
Akifungua mkutano huo, Kaduguda amewaomba radhi wanachama kwa uamuzi wake wa kutokugombea Uenyekiti na ataendelea kuwa mjumbe wa bodi.
“Niwaombe radhi kwa wale waliokuwa wananilaumu kuwa nimeegemea upande wa mwekezaji, lakini nilitumwa kuiongoza Simba na si kugombana na mwekezaji,” amesema Kaduguda huku akiwaomba wanachama kutumia fursa hiyo, kumchagua mmoja kati ya wanaogombea.
Leave a comment