KIUNGO mshambuliaji Raia wa Rwanda, Haruna Niyonzima, ataagwa rasmi ndani ya klabu ya Yanga tarehe 15 Julai, 2021, baada ya kuhudumu kwenye kikosi hiko kwa miaka saba. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezaji huyo ataagwa kwenye mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga wakiwa nyumbani dhidi ya Ihefu FC, utakaopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam, majira ya saa 10 jioni.
Taarifa hiyo imethibitishwa kupitia kurasa mbalimbali za mitandao ya kijamii ya klabu hiyo na kupitia kwa Afisa mhamasishaji na msemaji wa klabu hiyo, Antonio Nugaz ambaye aliandika kuwa “Tumuage kwa furaha na Amani fundi wa mpira Haruna Niyonzima.”
Mchezaji huyo kwa mara ya kwanza alikuja nchini mwaka 2012, akitokea klabu ya APR ya nchini Rwanda na kucheza Ligi Kuu Bara kwa miaka tisa, misimu saba akiwa na Yanga na misimu miwili katika klabu ya Simba.
Katika kipindi chote akiwa nchini Niyonzima ameshinda mataji matano ya Ligi Kuu Tanzania Bara, manne akiwa na Yanga na moja akipata wakati akikipa ndani ya klabu ya Simba.
Yanga wanakwenda kumuaga mchezaji huyo, mara baada ya kuonekana kuwa tayari kumuachia katika dirisha kubwa la usajili.
Leave a comment