AMANDUS Komba, mgombea ubunge Kawe jijini Dar es Salaam kupitia Chama cha TLP, amejigamba kuwaangushwa Halima Mdee (Chadema) na Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Jospehat Gwajima (CCM) katika uchaguzi mkuu utakaofanyika tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Komba ametoa tambo hizo leo Jumanne tarehe 25 Agosti 2020, baada ya kurudisha fomu ya uteuzi Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa Msimamizi wa Uchaguzi Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam.
Amesema, wananchi hawachagui majina ya watu bali watu watakaokwenda kuwatumikia na kwamba ana amini yeye sifa hizo anazo.
“Mdee na Askofu Gwajima nawaweza, mimi siendi kwenye uchaguzi wa wanaogombea kwa majina ya watu, mimi naenda kitumikia watu. Wananchi ndio watakaoamua. Mimi nawatumikia watu siangalii Gwajima wala Mdee,” amesema Komba.
Akielezea vipaumbele vyake, Komba amesema, wananchi wa Kawe wanakabiliwa na changamoto ya maji, migogoro ya ardhi na miundombinu ya barabara, hivyo masuala hayo ndio vipaumbele vyake endapo atafanikiwa kushinda uchaguzi huo.
“Vipaumbele vyangu wakinichagua kata ninayotoka kuna migogoro ya ardhi nitaanza kuitatua. Bunju kuna shida ya maji kama hatuna mbunge. Naona kata nyingi matatizo hayo yanajirudia rudia. Ya pili changamoto ya barabara, ya nne wakinichagua nitakua karibu yao sio kama wagombea wengine,” amesema Komba.
Shughuli ya uchukuaji na urudishaji fomu za kugombea katika uchaguzi huo lililoanza tarehe 5 Agosti 2020, linafungwa leo.
Pia, leo uteuzi wa wagombea unafanyika, huku kesho tarehe 26 Agosti, kampeni zitaanza na zitafungwa rasmi tarehe 27 Oktoba 2020 ambapo Jumatano ya tarehe 28 Oktoba 2020 utafanyika uchaguzi mkuu.
Leave a comment